Uhuru amteua mwenyekiti mpya wa NHIF - Lewis Nguyai

Muhtasari

• Rais pia alimteua Sitoyo Lopokoiyit kama mwenyekiti wa bodi ya Hospitali ya Rufaa ya Moi (MTRH).

Rais Uhuru Kenyatta
Rais Uhuru Kenyatta

Rais Uhuru Kenyatta amemteua Lewis Nguyai kuwa mwenyekiti wa Bodi ya Bima ya kitaifa ya Hospitali (NHIF).

Uteuzi huo ulifanywa katika ilani maalum ya gazeti la tarehe 23 Februari.

Nguyai atachukua nafasi ya Hannah Muriithi ambaye amekuwa msimamizi wa bodi hiyo tangu Aprili 2018.

 

Rais pia alimteua Sitoyo Lopokoiyit kama mwenyekiti wa bodi ya Hospitali ya Rufaa ya Moi (MTRH).

Anachukua nafasi ya mbunge wa zamani wa Eldoret Mashariki Joseph Lagat.

Lopokoiyit amekuwa akifanya kazi katika kampuni ya Safaricom tangu Aprili 2018, akiwa amewahi kuwa Mkurugenzi wa kitengo cha M-Commerce katika kampuni ya Vodacom Tanzania mwaka 2015.

Akiwa Afisa Mkuu wa Huduma za Fedha, alikuwa na jukumu la kukuza M-Pesa kuwa jukwaa kamili la kifedha.

Lopokoiyit anachukua majukumu yake tarehe 29 Machi.

Katika notisi hiyo, Rais pia alimteua Dkt Daniel Mbinda Musyoka kama mwenyekiti wa bodi ya Taasisi ya Utafiti wa matibabu ya Kenya (Kemri) na kufutilia mbali uteuzi wa Naftali Agata.

Mabadiliko katika NHIF yanajiri  wakati bima hiyo inatekeleza mpango wa Afya kwa Wote (UHC).