Kenya yaweka wazi kandarasi ya China ya ujenzi wa reli ya thamani ya $3bn

Uwezekano wa ujenzi wa reli hiyo umekuwa ukitiliwa shaka tangu ilipozinduliwa.

Muhtasari

•Kuweka wazi maelezo ya kandarasi hiyo ya reli ilikuwa mojawapo ya ahadi za Rais William Ruto katika kampeni ili kumaliza uvumi miongoni mwa Wakenya kuhusu kile ambacho serikali ilitia saini kwa niaba yao.

Mradi wa reli ya SGR ulifadhiliwa na serikali ya China
Image: BBC

Waziri wa uchukuzi wa Kenya ameweka hadharani nyaraka za mradi mkubwa wa reli ya Kenya uliotiwa saini na China baada shughuli hiyo kuendeshwa kwa usiri kwa miaka kadhaa.

Reli ya thamani ya $3bn (£2.6bn) inayofadhiliwa na China ni mradi mkubwa zaidi wa miundombinu nchini Kenya tangu nchi hiyo ilipopata uhuru wake mnamo 1963.

Uwezekano wake umekuwa ukitiliwa shaka tangu ilipozinduliwa.

Reli hiyo inapita kati ya mji wa bandari wa Mombasa na mji mkuu, Nairobi, na kuna mipango ya kuupanua hadi mji wa bandari wa Kisumu magharibi mwa Kenya.

Kuweka wazi maelezo ya kandarasi hiyo ya reli ilikuwa mojawapo ya ahadi za Rais William Ruto katika kampeni ili kumaliza uvumi miongoni mwa Wakenya kuhusu kile ambacho serikali ilitia saini kwa niaba yao.

Katika ujumbe wake wa twitter siku ya Jumapili, waziri Kipchumba Murkomen alisema nakala za makubaliano hayo ziwasilishwa viongozi kadhaa katika bunge la Kenya na pia kusambazwa na vyombo vya habari.

Taarifa za vyombo vya habari kuhusu mikataba iliyotolewa zinaonyesha kwamba wakopeshaji wa China walipewa mamlaka makubwa, ikiwa ni pamoja na kuhitaji usuluhishi wa mzozo wowote utakaofanyika Beijing, kulingana na gazeti la Daily Nation.

Mkandarasi mkuu wa mradi huo hakutozwa kodi zote, gazeti la Standard linaripoti.

Mnamo 2020, wizara ya mambo ya nje ya China ilikanusha madai kwamba bandari ya Mombasa, mojawapo ya bandari kubwa zaidi Kusini mwa Jangwa la Sahara, ilitumiwa kama dhamana katika makubaliano hayo.