Akuku Danger afichua mbona aliagiza kalamu na karatasi punde baada ya 'kufufuka' katika ICU

Muhtasari

•Akuku Danger alisema alipoteza fahamu yake alipokuwa amelazwa katika hospitali ya Nairobi Women's.

•Amefichua kwamba katika kipindi cha siku nne ambacho alikuwa amepoteza fahamu alijawa na vichekesho vingi akilini mwake,

Image: INSTAGRAM// AKUKU DANGER

Mchekeshaji wa Churchill Show, Mannerson Ochieng almaarufu Akuku Danger amekiri kwamba hafahamu kilichotokea  kati ya mwezi Desemba na Januari.

Akiwa kwenye mahojiano na Mpasho, Akuku Danger alisema alipoteza fahamu yake alipokuwa amelazwa katika hospitali ya Nairobi Women's.

"Nilikaa Nairobi Women's kwa siku tatu. Baada ya siku tatu nikapelekwa Nairobi West. Kati ya Nairobi Women's na Nairobi West siwezi kumbuka kilichoendelea kwani sikujipeleka pale. Nilikuwa nimezima. Sijui kilichofanyika Desemba yote na Januari yote," Alisema.

Mchekeshaji huyo alilazwa ICU kwa takriban siku nne, kipindi ambacho kulingana na maelezo yake, alikuwa 'amefariki'.

Amefichua kwamba katika kipindi cha siku nne ambacho alikuwa amepoteza fahamu alijawa na vichekesho vingi akilini mwake, vyote ambavyo aliandika chini punde baada ya fahamu yake kurejea.

"Kitu cha kwanza baada ya 'kufufuka', nilitaka kuandika. Niliagiza kalamu na karatasi. Akilini mwangu nilikuwa na vichekesho vingi na nilikuwa nacheka sana. Hayo yote yalifanyika katika kipindi ambacho nilikuwa nimezima. Sikuwa najua kilichokuwa kinaendelea lakini niliporudi niliagiza kalamu na karatasi. Niliandika vichekesho kadhaa, karatasi nzima. Nilitaka kuchekesha watu baada ya kurejea," Akuku Danger alisema.

Mchekeshaji huyo amesema kwamba hata baada ya fahamu yake kurejea ilichukua muda kabla yake kuanza kukumbuka vitu. Amefichua kwamba mwezi Februari ndipo alianza kukumbuka mambo kidogo kidogo.