Diamond ajawa bashasha baada ya bintiye Tiffah Dangote kukiri upendo mkubwa kwake

Tiffah alimwagia sifa kemkem baba yake na kukiri upendo wake usio na mwisho kwake.

Muhtasari

•Tiffah aliandika mfululizo wa jumbe akikiri kwa nini anampenda mwanamuziki huyo sana na kwa nini atamthamini kila wakati.

•Tiffah alieleza jinsi anavyoipenda sana familia ya Diamond akiwemo Mama Dangote na binti zake Esma Platnumz.

Diamond na Tiffah
Image: INSTAGRAM// PRINCESS TIFFAH

Bosi wa lebo ya WCB Diamond Platnumz ameonyesha fahari kubwa baada ya bintiye wa pekee, Tiffah Dangote kumsherehekea kwa upendo.

Tiffah ambaye ni mtoto wa kwanza wa staa huyo wa Bongo na mwanasoshalaiti  wa Uganda Zari Hassan alitumia akaunti yake ya WhatsApp kumwagia sifa kemkem baba yake na kukiri upendo wake usio na mwisho kwake.

Aliandika mfululizo wa jumbe akikiri kwa nini anampenda mwanamuziki huyo sana na kwa nini atamthamini kila wakati.

"Hii inaenda kwa baba yangu, nampenda sana. Yeye ndiye kila kitu changu. Ananipenda na atanipenda siku zote duniani kote. Ninampenda sana na atakuwa kila kitu changu kwa sababu nampenda sana. Pia baba yangu ananipenda sana," ujumbe mmoja ulisomeka.

Aliongeza,"Baba wewe ni malaika wangu milele katika ulimwengu mzima, unanipenda sana asubuhi hadi usiku."

Binti huyo mrembo mwenye umri wa miaka saba alibainisha kuwa Diamond anampenda pamoja na familia yote ya Zari Hassan. Pia alibainisha kuwa mwimbaji huyo wa Bongo ndiye mashuhuri  zaidi katika familia yao.

Tiffah pia alitengeneza ujumbe wa sauti akikiri jinsi mwanamuziki huyo anavyompenda yeye na familia yake. Pia alieleza jinsi anavyoipenda sana familia ya Diamond akiwemo Mama Dangote na binti zake Esma Platnumz.

Haya yanajiri siku chache baada ya binti huyo wa miaka 7 na kakake Prince Nillan kumtembelea baba yao nchini Tanzania. Wawili hao walirejea Afrika Kusini mwishoni wa mwezi Aprili baada ya kukaa Tz kwa siku kadhaa.

Diamond aliwasindikiza wawili hao hadi uwanja wa ndege walipokuwa wakirejea kwa mama yao takriban wiki mbili zilizopita. Alionyesha video kadhaa za kipindi cha kuagana chenye hisia katika uwanja wa ndege.

Katika video hizo, bosi huyo wa WCB alionekana akiwakumbatia wanawe kabla ya kuwapungia mkono wa kuwaaga.Binti yake, Tiffah hakuonekana kuwa tayari kumuacha na hata alilia huku akimpungia mkono wa kumuaga.

"Tutaonana, nakupenda, ni sawa, nitakuja, nitakuja," Diamond alimwambia binti yake huku akimuaga kwaheri.

Yeye pia alionekana kuwezwa na hisia huku akiondoka katika eneo la kuwaaga abiria la uwanja huo wa ndege.