"Nimepata ninayemtaka!" Paula Kajala akiri kuridhishwa na mapenzi ya Marioo

Mwanamitindo huyo alibainisha kuwa hatimaye amepata mpenzi wa ndoto yake.

Muhtasari

•Kajala amekiri mapenzi yake yasiyoisha kwa anayedaiwa kuwa mpenzi wake, mwimbaji Omary Mwanga almaarufu Marioo.

•Takriban wiki mbili zilizopita, Kajala alikiri hana uhakika iwapo binti yake  yupo anachumbiana na mwimbaji huyo.

Marioo akiwa na muhibu wake Paula.
Marioo akiwa na muhibu wake Paula.
Image: INSTAGRAM

Mwanamitindo wa Tanzania Paula Paul Kajala amekiri mapenzi yake yasiyoisha kwa anayedaiwa kuwa mpenzi wake, mwimbaji Omary Mwanga almaarufu Marioo.

Ijumaa, kwenye akaunti yake ya Snapchat, kipusa huyo mwenye umri wa miaka 20 alibainisha kuwa hatimaye amepata mpenzi wa ndoto yake.

Paula aliendelea kubainisha kuwa anafurahia sana mahusiano yake na mtunzi huyo wa kibao maarufu 'Mi Amor'.

"Nimepata mwanaume ninayemtaka, nina furaha," alichapisha.

Katika wiki chache zilizopita, binti huyo wa pekee wa muigizaji Kajala Masanja amedaiwa kuwa kwenye mahusiano na Marioo. Wawili hao wameonekana wakijivinjari pamoja na hata kuambiana maneno matamu ya mapenzi.

Haijabainika iwapokwa kweli wawili hao wanatoka kimapenzi ama ni kiki tu lakini kwa hakika wamekiri kupendana mara kadhaa.

Takriban wiki mbili zilizopita, muigizaji Kajala alikiri hana uhakika iwapo binti yake  yupo anachumbiana na mwimbaji huyo.

Akizungumza kwenye mahojiano na kituo kimoja cha redio cha humu nchini, mpenzi huyo wa zamani wa Harmonize aliweka wazi kuwa pia yeye anapata tetesi za mahusiano ya wawili hao kwenye mitandao ya kijamii.

"Sijui. Kwa kweli sijui chochote. Picha naziona tu kama wananchi wengine," alisema.

Paula alimtambulisha Marioo kama mpenzi wake mpya siku chache tu baada ya aliyekuwa mpenziwe, Rayvanny kuthibitisha kufufuka kwa mahusiano yake na mzazi mwenzake Fahyma almaarufu Fayvanny.

Bosi huyo wa Next Level Music alithibitisha kurudiana na Fahyma kwa kumshirikisha katika video ya wimbo wake 'Forever.'

“Mtoto mbichi teketeke aki Mama umelainika. Umeumbika, acha nikumwagie sifa. Waruke sakara na mateke uzuri wako hawatofika, mama umejazisha, mikate ya kumiminisha,” Rayvanny alimsfia Fahyma kwenye wimbo huo.

Takriban siku mbili baada ya kuachia wimbo huo, msanii huyo wa zamani wa WCB alithibitisha kuwa sasa hata wanaishi pamoja.

Rayvanny na Fahymah walitengana mwaka wa 2019 ambapo kila mmoja aliamua kuenda njia yake. Baada ya kutengana, haikumchukua Rayvanny muda mrefu kabla ya kuzama kwenye huba nzito na Paula. Wawili hao walianza kuchumbiana mwaka wa 2020.

Kwenye mahojiano ya hivi majuzi, Kajala alifichua kuwa hakufurahi wakati alipogundua  Paula yupo kwenye mahusiano na msanii huyo. Aliweka wazi kuwa pia yeye alikuja kufahamu kuhusu mahusiano hayo kupitia mitandao ya kijamii.

Alifichua kwamba alijaribu sana kumshauri mwanamitindo huyo mwenye umri wa miaka 20 dhidi ya mahusiano na bosi huyo wa Next Level Music lakini juhudi zake  ziliangukia patupu kwani Paula hakusikia.

"Nilijaribu sana kumweleza kwamba hii sio sahihi lakini mtu anaenda anafanya kinyume, inabidi umeacha tu. Ukimwambia asiende na huyo mtu anasema sawa lakini bado anaendelea. Nilijaribu kumzuia sana," alisema.

Aidha, alisema baada ya kushindwa kumshauri Paula dhidi ya uhusiano huo, alimshauri jinsi ya kujiendeleza katika mahusiano.