Mama Dangote ajigamba kuhusu mwanawe Diamond Platnumz kwa kununua ndege

Mama Dangote amemshukuru Mola na kujivunia mwanawe kwa mafanikio yake makubwa

Muhtasari

•Hivi majuzi Diamond alifichua kuwa tayari amenunua ndege ambayo alikusudia kununua kabla ya mwaka huu kuisha.

•Kufuatia ufichuzi huo, Mama Dangote amemshukuru Mola na kujivunia mwanawe kwa mafanikio yake makubwa.

Diamond na mamake Mama Dangote
Diamond na mamake Mama Dangote
Image: INSTAGRAM// MAMA DANGOTE

Mama Dangote ni mwanamke mwenye furaha tele kwa sasa kufuatia hatua ya mwanawe Diamond Platnumz kujinunulia ndege ya kibinafsi.

Hivi majuzi Diamond alifichua kuwa tayari amenunua ndege ambayo alikusudia kununua kabla ya mwaka huu kuisha.

"Wakati mwingine kwa mtu kama mimi ambaye alitoka mtaani nikinunua gari yenye thamani dola milioni moja, mtu mwingine atashangaa ni ya kazi gani. Lazima nifanye hivo, nisipofanya hivo hawatanithamini.Mwingine ataonekana kama yeye ndiye staa ilhali siye. Kusema kweli hata nimenunua ndege sasa," Staa huyo wa Bongo alisema katika mahojiano ya hivi majuzi na DW Afrika.

Kufuatia ufichuzi huo, Mama Dangote amemshukuru Mola na kujivunia mwanawe kwa mafanikio yake makubwa.

"Alhamdulilaah, Mungu Mkubwa Keo hii unamiliki ndege Naseeb," Mamake Diamond alisema kupitia Instastori zake.

Diamond ambaye anaaminika kuwa mmoja wa wasanii tajiri zaidi Afrika alitangaza mpango wake wa kununua ndege takriban miezi miwili iliyopita .

Bosi huyo wa WCB alitangaza kuwa angekuwa mmiliki wa ndege la kibinafi kufikia mwisho wa mwaka huu.

"Tulinunua 2021 Rolls Royce Black Bedge Zero Kilometre mwaka jana, na tunanunua ndege ya kibinafsi mwaka huu!! hiyo ndio tafsiri ya kuwa na usimamizi bora!! Ni Siku ya Kuzaliwa ya meneja wangu Sallam Sk," Aliandika kwenye Instagram mwezi Mei.

Mwanamuziki mkongwe wa Bongo Baba Levo pia alikuwa amedokeza kuhusu mpango huo wa mwandani wake.

"Nasema hivi! Ikifika mwezi wa kumi kama Diamond hajanunua ndege niuawe," Levo alisema mapema mwaka huu.