"Acha kuniambia nipumzike kila wakati, inakera!" Diana Marua amlalamikia mume wake Bahati

Rapa huyo alieleza kusikitishwa kwake na hali yake na kudai anahisi kama amekuwa mzigo tu nyumbani.

Muhtasari

•Diana amebainisha kuwa mwanamuziki huyo amekuwa akitia juhudi kubwa kuhakikisha familia  yao iko sawa.

•Diana amesema kwamba amechoshwa na starehe aliyonayo sasa na anayatamani sana maisha yake ya kawaida.

Bahati na mkewe Diana Marua
Image: INSTAGRAM// DIANA MARUA

Mwanavlogu Diana Marua ametoa shukrani za dhati kwa mume wake Bahati kwa usaidizi ambao ameendelea kumpa katika safari yake ya ujauzito.

Katika ukurasa wake wa Instagram, amebainisha kuwa mwanamuziki huyo amekuwa akitia juhudi kubwa kuhakikisha familia  yao iko sawa.

"Nakushukuru Bahati. Asante kwa kufanya kila uwezalo kunifanya mimi na watoto tuwe starehe," alisema siku ya Alhamisi.

Mama huyo wa watoto wawili alidokeza kuwa ujauzito wake wa tatu umekuwa wa kuchosha sana. Alibainisha kuwa mumewe amekuwa akimtaka apumzike sana, jambo ambalo hafurahishwi nalo tena.

"Acha kuniambia nipumzike kila wakati, inakera. Nimepumzika kutosha lakini bado nimechoka. Lol, Nakupenda," alimwambia Bahati.

Diana alieleza kusikitishwa kwake na hali yake ya sasa na kudai anahisi kama amekuwa mzigo tu katika nyumba yake.

Aidha amesema kwamba amechoshwa na starehe aliyonayo sasa na anayatamani sana maisha yake ya kawaida.

"Weeeuuuhhh, semeni KUBEAT!!!! Kusema nimechoka ni dharau. Nimemiss kwenda kazini. Ninahisi kama sichangii chochote ndani ya nyumba. Ninakaa tu, kula, kunywa, kulala na mzunguko unaendelea 😔,

Haya yanajiri huku rapa huyo akitarajiwa kujifungua mtoto wake wa tatu wakati wowote hivi karibuni.

Mapema mwezi huu mwanavlogu huyo  alitangaza kuwa ujauzito wake ulikuwa katika kipindi cha mwisho. Alidokeza mabadiliko kadhaa ambayo ameshuhudia mwilini na kufichua safari ya ujauzito haijakuwa rahisi.

"Kuna wakati kuamka kitandani haikuwa kazi ngumu, niliweza kulala kwa nafasi yoyote, nakosa kulala juu ya tumbo langu.

Kuna wakati niliweza kutoshea saizi ya kiatu changu bila shida yoyote. Miguu yangu sasa inashindana na ile ya tembo," alisema.

Pia alibainisha hawezi kuwa bafuni kwa muda mrefu na kuoga kwa muda mrefu kwa sababu hataki tena maji ya moto.

Hapo awali Bahati alikuwa amedokeza kuwa tarehe ya mkewe kujifungua imekaribia sana.

Alitoa tangazo hilo alipokuwa akiwahutubia mashabiki wake katika tamasha la Wamusyi Night lililofanyika wiki chache zilizopita.

"Diana anatarajia kujifungua dakika yoyote sasa!"  alisema.

Mwimbaji huyo alisema amekuwa akikaa karibu na mkewe mara nyingi kwa sababu anaweza kupata uchungu wa leba wakati wowote.

"Lazima nikae karibu na nyumbani," alisema.

Wanandoa hao ambao wamekuwa pamoja kwa takriban miaka sita wanatarajia mtoto wao wa tatu pamoja. Tayari wana mtoto mmoja wa kike na mwingine wa kiume pamoja, Heaven Bahati na Majesty Bahati.