Diamond aweka wazi kilichovunja mahusiano yake na Zuchu

Yote yalianza kwa Zuchu kutangaza yuko single na ameumizwa moyoni.

Muhtasari

•Matendo  ya hivi punde ya Diamond na Zuchu kwenye mitandao ya kijamii yameibua wasiwasi kuhusu mahusiano yao.

•Diamond alidokeza kuwa mpenziwe amekuwa akijinufaisha na yeye kwa sababu ya mapenzi yake makubwa kwake.

katika ziara yao ya Ufaransa.
Diamond Platnumza na anayedaiwa kuwa mpenziwe, Zuchu katika ziara yao ya Ufaransa.
Image: INSTAGRAM// ZUCHU

Huenda mambo yameharibika kwenye mahusiano ya mastaa wawili wa bongo wanaoamika kuwa wapenzi, Diamond Platnumz na Zuchu.

Matendo yao ya hivi punde kwenye akaunti zao za mitandao ya kijamii yameibua wasiwasi mkubwa miongoni mwa wafuasi wao  wengi ambao wamekuwa wakifuatilia na kushabikia uhusiano wao wa zaidi ya mwaka mmoja.

Yote yalianza kwa Zuchu kutangaza kwamba sasa yuko single na ameumizwa moyoni.

"Single.." aliandika kwenye akaunti yake ya mtandao wa Snapchat na kuambatanisha na emoji ya moyo uliovunjika '💔'

Binti huyo wa gwiji wa taarab, Khadija Kopa aliendelea kuchukua hatua ya kufuta picha na video zote za bosi huyo wake ambaye kwa muda mrefu imekuwa ikidaiwa kuwa yuko na uhusiano wa kimapenzi naye.

Diamond aliendelea kuongeza wasiwasi miongoni mwa mashabiki wao huku akichapisha ujumbe wa kimafumbo kwenye ukurasa wake wa Instagram ambao ulionekana kuzungumzia uhusiano wake.

Bosi huyo wa WCB alikubaliana na maneno ya meme iliyosomeka, “Muweke mpenzi wako mbele na umuone akianza kukutumia vibaya.

Kwa chapisho hilo, Diamond alionekana kudokeza kuwa Zuchu amekuwa akijinufaisha na yeye kwa sababu ya mapenzi yake makubwa kwake.

Wawili hao hata hivyo hawajathibitisha wasiwasi huo wala kutoa maelezo zaidi kuhusu kile kinachoendelea kati yao.

Kabla ya kuchukua hatua tatanishi ya kufuta picha zote za Diamond kwenye ukurasa wake wa Instagram, mtunzi huyo wa kibao 'Sukari' alichapisha picha mbili nzuri zake akiwa na bosi huyo wake.

Kando ya picha hizo, alichapisha sehemu ya wimbo wake mpya  'Utaniua' na kuongeza tetesi za uhusiano mkubwa kati yao.

"Tukikosa stuli ni sunna kula kwenye mkeka. Unijue vizuri nkinuna mie ndo nadeka. Usije dhani kiburi uniache nkaja kuchekwa. Baby raha ya shughuli mkunwa awe na hekaheka," aliimba katika sehemu aliyoshiriki.

Takriban wiki mbili zilizopita, Diamond aliwasisimua wanafamilia wake huku akimtambulisha msanii huyo wake kama mke wake wakati wa karamu ya kusherehekea siku ya kuzaliwa ya dada yake mkubwa Esma.

Baada ya kutoa hotuba yake kwenye karamu hiyo, bosi huyo wa WCB alimwalika Zuchu na kumtabulisha kama mwenzi wake.

"Sasa mwenzangu Zuhura akasema angependa sana tukuje pamoja. Sasa mimi ni shabiki wa maagizo naomba aje awasilishe," Diamond alisema huku chumba cha sherehe kikijawa na shangwe na nderemo.

Kabla ya kuondoka jukwaani na kuchukua nafasi yake, mwimbaji huyo pia alimtaja Zuchu kama  wifi wa dada yake Esma.

"Hapo ndipo tutajua kama ana mapenzi na wifi wake," alisema.

Wahudhuriaji wa karamu hiyo walionekana kufurahishwa sana na utambulisho wa Diamond kwa Zuchu, ishara ya wazi kuwa wengi wao wameidhinisha uhusiano kati ya wawili hao na wapo tayari kushuhudia ndoa.