Ukiahiri ninaahiri! Harmonize azidi kumganda Diamond

Muhtasari

• Baada ya Diamond kutangaza kuahirisha kuachia EP yake kutoka Machi 4 hadi Machi 11, Harmonize naye anasemekana kuahirisha kuachia ngoma yake ya Bakheresa kutoka Machi 4 hadi Machi 12.

Harmonize na Diamond
Harmonize na Diamond
Image: INSTAGRAM

Msanii Harmonize bado anazidi kuwa kovu la kudumu katika maisha ya kimuziki ya Diamond Platnumz. Hii ni baada ya Harmonize kuzidi kumganda Diamond kwa kile anachotangaza kukifanya kimuziki na Harmonize naye hutangaza vivyo hivyo.

Ikumbukwe mwezi jana Diamond alikuwa ametangaza kuachia EP yake tarehe 4 mwezi Machi na Harmonize naye akaibuka na kutangaza tarehe hiyo hiyo kuwa ndio siku alikusudia kuachia kibao chake kipya ambacho alikitaja kuwa cha mwaka, kwa jina la Bakhresa.

Baadae wiki jana hivi Diamond tena akatangaza kuhairisha tarehe ya kuachia EP yake hadi tarehe 11 Machi na cha kushangaza ni kwamba pia Harmonize ametoa tangazo la kughairisha tarehe ya kuachia kibao chake cha mwaka hadi tarehe 12 Machi.

Mikwaruzano ya wawili hawa inaendelea chini kwa chini huku taarifa zikisema kwamba Diamond alifanya kusogeza siku ya kuachia EP yake wiki moja mbele kutokana na kwamba Harmonize alikuwa na tamasha kubwa la Afro East Carnival siku moja mbele ila wengi wameshindwa kuelewa ni kwa nini Harmonize ameamua pia kutoa kibao chake tarehe 12, siku moja baada ya EP ya Diamond.