(Video) Produsa Motif afurahia kushiriki kwenye promo ya albamu ya DJ Khaled

DJ Khaled aliwataka mashabiki wake wote kushiriki katika promo ya albamu yake ambapo walimtumia video fupi akaziunganisha na kupakia.

Muhtasari

• Wakenya wengi walimpongeza Motif kwa kuiwakilisha Kenya katika promo ya albamu ya DJ Khaled.

Mzalishaji maarufu nchini wa midundo ya Gengetone na Rap, Motif amekosha nyoyo za wakenya wengi wapenda Sanaa ya humu nchini baada ya kuonekana kwenye promo ya albamu mpya ya msanii maarufu kote ulimwenguni, DJ Khaled.

Msanii huyo kutokea Marekani ambaye pia anajiongeza kama mcheza santuri yupo katika maandalizi ya kuachia albamu yake ya kumi na tatu katika safari ya muziki wake na aliwataka mashabiki wake kutoke kote ulimwenguni kumtumia video yao ya sekunde kiasi wakiifuatisha kwa maneno ‘   God Did’ ambalo ndilo jina la albamu yenyewe.

“MUNGU ALIFANYA - KWA ULIMWENGU 🌎 #FANLUV endelea kutuma video zako ndani!!post na #GODDID. ALBUM MPYA INAKUJA HIVI KARIBUNI,” aliandika DJ Khaled.

Katika video aliyoipakia msanii huyo, alitanguliza kwa neno la ‘Hawakutuaminia’ ambapo mashabiki wake walifaa kumalizia usemi huo katika video fupi ambazo wangetuma.

“….ila Mungu alituaminia,” Motif anaonekana akimalizia usemi huo akiwa na Wamaasai katika hifadhi ya Wanyama pori ya Nairobi.

Wakenya walifurahikia kuwakilishwa vizuri na Motif katika video hiyo ya Khaled ambayo imeshirikisha watu zaidi ya kumi kutoka mataifa mbali mbali ulimwenguni.

Motif ni produsa mkubwa nchini anayejulikana pakubwa kutokana na kupiga midundo yake haswa kwenye ngoma nyingi za msanii wa kufoka na kuchana mistari, Khaligraph Jones.

Akitangaza jina rasmi la albamu hiyo, msanii DJ Khaled alisema kwamba aliiunda kwa watu wote wakiwemo wanaoamini Mungu na wasioamini Mungu.

Alidokeza kwamba albamu hiyo inashirikisha majina makubwa kama vile kina Drake, Kanye West, Lil Baby, Lil Durk, Future, Don Toliver, Roddy Ricch, Gunna, na 21 Savage, miongoni mwa wengine.