Jaribu kuvaa vizuri nione kama nitakufikiria - Mbunge Salasya amwambia Manzi wa Kibera

Salasya alimwambia kwamba watu ambao anawawakilisha bungeni ni watu makini sana kwa uvaaji wa mwanamke atakayemuoa.

Muhtasari

• Hao watu ninaowahudumia ni makini sana kwenye uwasilishaji wa picha ya mtu nitakayemuoa - Mbunge Salasya.

Mbunge Salasya amtaka Manzi wa Kibera kuvalia vizuri
Mbunge Salasya amtaka Manzi wa Kibera kuvalia vizuri
Image: Twitter

Baada ya kimya cha muda mrefu, hatimaye mwanasosholaiti Manzi wa Kibera amejitokeza tena na safari hii akituma ombi lake kwa mbunge wa Mumias East Peter Salasya kumfanya mke wake.

Manzi wa Kibera alionekana katikati ya jiji la Nairobi akiwa ameinua bango juu lenye ujumbe kwa mheshimiwa Peter Salasya akitaka kuwa mke wa mheshimiwa huyo kijana.

Salasya ambaye ndio mara yake ya kwanza kuchaguliwa kama mbunge amevutia maombi kadhaa kutoka kwa kina dada ambao wanataka kupata nafasi kuolewa na yeye, haswa baada ya kutangaza hadharani kwamba anatafuta mke.

“Mheshimiwa Peter Salasya, nioe tafadhali,” ujumbe kwenye bango hilo ulisoma huku ukiambatanishwa na nambari yake ya simu.

Ikumbukwe mapema wiki hii pia mwanadada mmoja kwa jina Lydia Richard alionekana na bango kama hilo akitaka kuwa mke wa mbunge Salasya, hatua ambayo ilimfanya Salasya kumpa mwaliko rasmi katika majengo ya bunge ambapo walishiriki chakula cha mchana pamoja.

Salasya pia baada ya kuona bango hilo la Manzi wa Kibera, alijibu kwa kusema kwamba pia atamzingatia na kumtaka kwanza kuvalia mavazi ya heshima.

“Wakati mwingine ukibeba bango jaribu kuvaa kitambaa cha heshima angalau najivunia wewe na wakenya kwa ujumla. Hao watu ninaowahudumia ni makini sana kwenye uwasilishaji wa picha ya mtu nitakayemuoa. Manzi wa Kibera nakutakia kila la kheri. Siku moja nitakuja tushirikiana pamoja katika ibada kanisani,” alisema.

Salasya alisema wanadada hao wawili ambao wametupa ndoana kwake wote ni wazuri kwa kiasi chake na kutania kwamba atafungua kanisa nao na kusema Lydia atakuwa msimamizi wa kitengo cha nyimbo za kuabudu huku Manzi wa Kibera akiwa kama mkaribishaji.

“Dada zangu wawili hapa chini ni mabinti wa ajabu wa nchi hii. Nimeongea na wote wawili na wako sawa na wanafuraha. Nimewaahidi kuwa tutafungua kanisa. Lydie Ronad atasimamia kusifu na kuabudu naye Manzi wa Kibera atakakuwa mtu wa kukaribisha waumini kanisani, na mimi nitakuwa mhubiri, ama niaje wadau,” Peter Salsya aliandika Twitter.