Zuchu adaiwa kuiba staili na kibwagizo cha wimbo wa injili, akabiliwa na shtaka kubwa

Ngoma ya 'Kwikwi' ilisemekana kukariri staili na kibwagizo kutoka kwa wimbo wa injili wa 'Wema wa Mungu' wake msanii Enock Jonas.

Muhtasari

• Msanii Jonas alisema alipotaarifu uongozi wa WCB kuhusu suala hilo, walimkandia na kumwambia kwa jeuri kwamba hata milioni 2 hawezi akafidiwa.

Zuchu adaiwa kuiba wimbo wa injili wa Enock Jonas
Zuchu adaiwa kuiba wimbo wa injili wa Enock Jonas
Image: Instagram

 Msanii Zuhuru Othman maarufu Zuchu amejipata pabaya baada ya kudaiwa kuimba baadhi ya mistari kwenye wimbo wa injili wa msanii Enock Jonas.

 

Tarifa zilizopo ni kwamba msanii huyo malkia kutoka lebo ya WCB Wasafi alitumia kionjo pamoja na mtindo wa wimbo kwa jina ‘Wema wa Mungu’ pasi na kupewa idhini na mwenyewe, msanii Enock Jonas.

 

Kufuatia ufichuzi huo, huenda Zuchu akazama mkobani pake na kutengana na kima cha shilingi milioni 500 za Kitanzania ambazo ni sawa na milioni 25 pesa za Kenya.

 

Katika malalamiko hayo Jonas, alisemekama kudai Zuchu alichukua sehemu ya kibwagizo na staili ya kucheza katika wimbo wake wa 'Wema wa Mungu' ambao ulitoka mwaka 2012 lakini ulijulikana zaidi kwa jina la 'Zunguka'.

 

Taarifa za madai hayo zilianza kusambaa mitandaoni kupitia barua iliyoandikwa na kampuni inayojihusisha na masuala ya hati miliki, Gerpat Solution, ambapo mwasisi wake Gerlad Magubuka, alinukuliwa na jarida la Mwananchi nchini humo kuwa Jonas alienda kwao kulalamika baada ya kusikia wimbo wa Zuchu kwa jina ‘Kwikwi’ ambo umekuwa ukifanya vizuri sana mitandaoni wiki mbili tangu kutoka.

 

Katika wimbo huo ambao bado video halisi haijatoka, Zuchu alipakia video akisakata densi na timu ya wacheza densi wake na ndio tuhuma zimeibuliwa kuwa mtondo huo wa usakataji pamoja pia na kiradidi cha ‘Zunguka’ kimesemekana kuibwa kutoka kwa Jonas.

 

“Magabuka amesema tayari wameshawapelekea wahusika barua ya madai hayo na nakala nyingine wamepeleka Taasisi ya Hakimiliki Nchini (Cosota) na Shirikisho la Wanamuzi Tanzania (Shimuta),” Mwananchi waliandika.

 

Akizungumza na Mwananchi, Enock amesema amelazimika kuchukua hatua hiyo baada ya mazungumzo na upande wa Zuchu kushindikana kwa kumwambia kuwa katika madai hayo hata Shilingi milioni 2 za Kitanzania hawawezi kumlipa.

Amesema majibu hayo alipewa na mmoja wa mameneja katika lebo ya Wasafi, Khamis Taletale (Babu Tale), baada ya kuzungumza naye kwa njia ya simu siku ya Jumanne.

 

‘Kwikwi’ mpaka sasa una watazamaji zaidi ya milioni 4 kwenye mtandao wa YouTube ilhali wimbo wa Enock Jonas ‘Wema wa Mungu’ una watazamaji laki tatu na ushee tu!