Jumbe za heri njema kwa Bahati na mkewe Diana kwa kujaliwa mtoto wa 3

Diana Marua alijifungua wiki hii Jumanne Novemba tarehe 1

Muhtasari

• Katika kurasa zao za Instagram, watu maarufu hawakusita kuwapongeza Diana na Bahati.

• Wawili hao walibarikiwa na mtoto msichana siku ya Jumanne na kumuita Malaika Nyambura Bahati.

Bahati na Diana Marua wamkaribisha binti yao duniani

Mwanamuziki Bahati na mkewe Diana Marua wamejaliwa na mtoto wa tatu. Walitangaza kuwa mama huyo amejifungua juzi Jumanne Novemba tarehe1.

Wawili hao walibarikiwa na mtoto msichana siku ya Jumanne na kumuita Malaika Nyambura Bahati.

Mastaa hao wawili wa mziki wa kizazi kipya walipokea jumbe za heri njema  mtandaoni na mashabiki wao wakiwemo watu mashuhuri.

Baadhi ya maoni hayo ni kama:

"Hongera @diana_marua na @bahatikenya 🎊 👏 💐 team Dee. Hatimaye jina  niliopendekeza lilishinda nyoyo zao🏆 🙌 👏 baby @malaika_bahati karibu duniani 🌎 Tunakupenda sana❤️ aki nazidi kutamani mtoto sasa😢karibu nikuimbie karibu kenya hakuna matata😍," Saraha Kabu alisema.

"Hongera sana. Azidi kupata mapendekezo kutoka kwa Mungu na wanadamu," Kabi Wajesus alisema.

"Hongera Baba Nyambura," mwanamuziki Nameless alimpongeza Bahati.

Hata rafiki yake wa karibu alikuwa miongoni mwa watu waliowatakia heri njema.

"Hongera sana 🍾🎊🎉,'" Dkkwenyebeat alisema.

Wapenzi hao walitangaza siku ya Jumanne kuwa Diana alikuwa hospitalini tayari kujifungua .

Bahati alimuomba Mungu amlinde mke wake katika hatua muhimu iliyo mbele yake.

"Malkia ameingia hospitalini katika Wodi ya Kujifungua. Mungu amtangulie," alisema huku akiambatanisha ujumbe huo na picha ya mkewe akiwa amekalia kitanda cha hospitalini kwa wodi ya wazazi.

"Kwa Binti Yangu💓... Ni Wakati, najua kuwa utakuwa hapa dakika yoyote kuanzia sasa lakini jambo la kusikitisha ni kwamba Baba na Mama yako bado hawajatafuta jina zuri kwa ajili yako Princess 🤦‍♂️🤦‍♀️," Bahati aliandika.

Mashabiki wao wamekuwa wakionyesha dalili za kuchoshwa na habari za wanandoa hao za kujifungua kila kuchao.

Walidai kuwa Diana amekuwa akitafuta kiki kupitia uja uzito wake na kusema kuwa mama huyo alikuwa ashajifungua mwezi uliopita.