Vincent Mboya adai TikTok imegeuka kuwa jukwaa la omba-omba, “Kila mtu anaomba gifts!”

Mboya alisema kwamba tiktok inafaa kuwa jukwaa la kuburudisha wale wanaokushabikia na wala si kugeuza mashabiki wako kuwa kitega uchumi chako, kila wakati ukienda ‘live’ kazi ni kuomba ‘gifts’ badala ya kuwaburudisha wanaokutazama.

Muhtasari

• Kauli ya Mboya inakuja siku chache baada ya baadhi ya Wakenya kumshtumu pasta Kanyari kwa kuingia TikTok kwa sababu ya pesa.

• Hata hivyo, Kanyari akizungumzia suala la kuingia tiktok kwa sababu ya pesa, alikanusha hilo akisema kwamba alijiunga tiktok ili kuwakomboa vijana ambao wameshikiliwa na ibilisi.

Vincent Mboya
Vincent Mboya
Image: Instagram KWA HISANI

Mwanablogu wa YouTube aliyeahmia Kanada, Vincent Mboya amewasuta vikali tiktokers ambao sasa anadai wamegeuza jukwaa hilo la video fupi kuwa jukwaa la omba omba.

Kupitia instastory yake, Mboya alidai kwamba TikTok mwanzoni ulikuwa ni mtandao wa kufurahisha watu kwa video fupi lakini tiktokers wengi wa Kenya kwa sasa wanatumia jukwaa hilo kuomba mashabiki wao zawadi badala ya kufanya kazi.

Mboya alisema kwamba tiktok inafaa kuwa jukwaa la kuburudisha wale wanaokushabikia na wala si kugeuza mashabiki wako kuwa kitega uchumi chako, kila wakati ukienda ‘live’ kazi ni kuomba ‘gifts’ badala ya kuwaburudisha wanaokutazama.

“Maceleb wa Kenya sasa imetosha, achene kuwatumia vibaya Wakenya na roho yao nzuri ya kutoa. Kama usanii umekataa, nendeni mfanye kazi, acha kuwa omba omba mchango. Na kama hauna kazi rudi kijijini. Kuingia tiktok live na kuomba gifts hiyo sio kazi,” Mboya alisema.

Mwanablogu huyo alitoa mfano jinsi mtandao huo ulikuwa wa burudani nzuri nyakati za mwanzoni na watu wa awali kama kina Azziad Nasenya, akisema kuwa hao ndio walikuwa wapakuaji wa burudani bila kuwalipisha mashabiki wao.

“TikTok ilikuwa ni furaha tupu kabla ya siku za kina Azziad, lakini siku hizi kila mtu tiktok ni ombaomba, tafakari wajinga sisi ambao tunatuma hizo zawadi, hebu na tugutuke kutoka usingizi na tuwalazimishe tiktokers hawa watuburudishe na sio kuwa ombaomba,” Mboya alisema.

Kauli ya Mboya inakuja siku chache baada ya baadhi ya Wakenya kumshtumu pasta Kanyari kwa kuingia TikTok kwa sababu ya pesa.

Kanyari alijiunga kwenye mtandao huo hivi majuzi na amekuwa akifanya vipindi mubashara huku akiwasisitizia kwa kuwaomba mashabiki wake kumtumia zawadi kwa wiki.

Hata hivyo, Kanyari akizungumzia suala la kuingia tiktok kwa sababu ya pesa, alikanusha hilo akisema kwamba alijiunga tiktok ili kuwakomboa vijana ambao wameshikiliwa na ibilisi.

 “Sipo hapa kwa sababu ya pesa. Sipo hapa kwa sababu ninapokea zawadi. Niko hapa kwa sababu napenda TikTok na ninataka kuwaombea wagonjwa na watoto. Kuna watu wanaonewa na shetani, wengine wana matatizo, na wengine wanaishi nje ya nchi lakini hawana furaha. Niko hapa kuwaombea watu hao,” alisema.