Mchungaji taabani kwa kunajisi msichana wa miaka 6 Kawangware

Muhtasari

•Mhasiriwa alikuwa ameenda nyumbani kwa mchungaji huyo ili kupata mafunzo ya urembo   utoka kwa mke wake wa pili.

•Wakili alisema mshtakiwa ni mtu wa Mungu anayetumikia kanisa la mitume la African Green Cross.

Michael Masinde, mtu wa Mungu anayeishi Kawangware
Michael Masinde, mtu wa Mungu anayeishi Kawangware
Image: CLAUSE MASIKA

Mchungaji mmoja ameshtakiwa kwa kumnajisi msichana wa miaka sita nyumbani kwake katika mtaa wa Kawangware.

Michael Masinde alishtakiwa mbele ya hakimu William Tulel wa mahakama ya Kibera na kukanusha mashtaka.

Mhasiriwa alikuwa ameenda nyumbani kwa mchungaji huyo ili kupata mafunzo ya urembo   utoka kwa mke wake wa pili.

Inasemekana alitenda kosa hilo mnamo Machi 25 katika eneo la Stage  56, kaunti ndogo ya Dagoretti, kaunti ya Nairobi.

Kulingana na ripoti ya upelelezi, msichana huyo alikuwa anacheza na rafiki yake wakati mshtakiwa alimpa rafikiye pesa aende kununua biskuti kisha akatumia fursa hiyo kumwita nyumbani kwake.

Msichana huyo alipoenda pale, mchungaji huyo alifunga mlango kwa ndani, akamvua nguo, akamnajisi kisha akampa pesa na kumwambia asilie wala kumwambia mtu yeyote.

Baada ya kuondoka nyumbani kwa mchungaji huyo, mhasiriwa anasemekana kupata shida ya kutembea na wavulana wawili ambao  nao njiani walimwona na kuripoti.

Mchungaji alikamatwa na kupelekwa katika kituo cha polisi kabla ya kufikishwa mahakamani.

Hata hivyo kupitia kwa wakili wake Robert Businge, mshukiwa aliitaka mahakama kumwachilia kwa bondi.

Businge alisema mshtakiwa ni mtu wa Mungu anayetumikia kanisa la mitume la African Green Cross.

Hakimu alimwachilia kwa bondi ya Sh500,000 na kuamuru kesi hiyo isikilizwe Aprili 13.