Sakaja awakosha watu kwa Kiswahili, amtambua DP Gachagua kama mtoto wa Mau Mau

Sakaja alianza hotuba yake kwa lugha ya Kiswahili ambacho kilimtiririka kwa ufasaha, jambo ambalo liliwafurahisha wengi.

Muhtasari

• Sakaja alimkaribisha naibu rais Rigathi Gachagua na kusema kwamba pia yeye ni shujaa ambaye ni mtoto wa Mau Mau

Gavana wa Nairobi , Johnson Sakaja
Gavana wa Nairobi , Johnson Sakaja
Image: Facebook

Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja amewakosha Wakenya wengi baada ya kutoa hotuba yake katika sherehe za mashujaa kwa lugha ya Kiswahili.

Sakaja ambaye alikuwa kiongozi wa kwanza kutoa hotuba yake alitumia Kiswahili kilichonyooka, jambo ambalo lilimpa sifa tele kutoka kwa wanamitandao ambao walimsifia kwa kukumbatia lugha hiyo ya Kiafrika.

Sherehe za mashujaa ziliandaliwa katika uwanja wa Uhuru Gardens jijini Nairobi na gavana Sakaja aliwatambua watu mbali mbali kama mashujaa amabo wanafaa kusherehekewa.

Aliwaambia Wakenya kwamba leo hii watakapotoka mahali na kuwakuta maafisa wa polisi, walimu, madaktari miongoni mwa wengine, wote hao ni mashujaa na wanafaa heshima kubwa.

“Ukimuona polisi, ukimuona daktari,ukimuona mwalimu, hao wote ni mashujaa na wanahitaji kuheshimiwa,” Gavana Sakaja alizungumza kwa lugha ya Kiswahili sanifu.

Pia alichukua fursa hiyo kumkaribisha naibu wa rais Rigathi Gachagua ambaye alimtambua kama mtoto wa Mau Mau ambaye pia ni shujaa kulingana na maneno ya gavana huyo wa Nairobi.

Ufasaha wake katika lugha ya Kiswahili ulipungiwa mkono wa kongole, haswa ikizingatiwa kwamba alipigwa vita vikali na baadhi ya viongozi waliozua dhana kwamba huenda hakuwa na cheti cha digrii, ambacho ndicho kilikuwa kigezo kikubwa kwa mgombea kuruhusiwa kugombea urais.

Licha ya vizingiti hivyo vyote, Sakaja alijikaza na kushinda ugavana wa jiji kuu ambalo ni kitovu cha uchumi wa Kenya kupitia tikiti ya chama tawala cha UDA huku akimbwaga mpinzani wake mkuu Polycarp Igathe aliyekuwa akimenyana naye kwa tikiti ya chama cha Jubilee.