"Wakili wangu atakuwa jua na mwezi" Yesu wa Tongaren asema baada ya kujiwasilisha kwa polisi

"Huenda wakili wangu atakuwa jua na mwezi maana sina dhambi yoyote ya makosa juu ya wanadamu," alisema.

Muhtasari

•Bw Simiyu aliandamana na kundi la wafuasi wa kanisa lake alipojiwasilisha katika afisi za mkuu wa polisi wa Bungoma Bw Kooli.

"Tangu nianze kufanya kazi hii ya Mungu nikiwa na miaka 30, leo niko na miaka 42, sijawahi kuona kosa ambalo nimefanya," alisema.

akizungumza na waandishi wa habari alipojiwasilisha mbele ya mkuu wa polisi wa Bungoma Francis Kooli mnamo Mei 10, 2023.
Yesu wa Tongaren akizungumza na waandishi wa habari alipojiwasilisha mbele ya mkuu wa polisi wa Bungoma Francis Kooli mnamo Mei 10, 2023.
Image: SCREENGRAB

Mhubiri wa Bungoma mwenye utata Eliud Simiyu almaarufu Yesu wa Tongaren ameweka wazi kuwa hana hatia yotote dhidi ya wanadamu.

Siku ya Jumatano, mwanzilishi huyo wa kanisa la New Jerusalem katika eneo la Tongaren alitimiza agizo la kujiwasilisha katika ofisi za bosi wa polisi wa kaunti ya Bungoma Francis Kooli ambapo alibainisha hajatenda kosa lolote.

"Mimi najua kuwa sheria hushika wale ambao wana kosa," Bw Simiyu aliwaambia waandishi wa habari nje ya ofisi za Bw Kooli.

Aliongeza, "Tangu nianze kufanya kazi hii ya Mungu nikiwa na miaka 30, leo niko na miaka 42, sijawahi kuona kosa ambalo nimefanya."

Mchungaji huyo alidokeza kwamba kila siku anaongozwa na Mungu ambaye huhakisha hajaenda kinyume cha matakwa yake kwake.

Alipoulizwa iwapo amejipanga na timu ya mawakili iwapo kutapatikana kesi dhidi yake, mhubiri Yesu wa Tongaren alisema wazi kuwa, "Huenda wakili wangu atakuwa jua na mwezi maana sina dhambi yoyote ya makosa juu ya wanadamu. Nikisema jua, nitawaachia kitendawili hicho mtategua."

Bw Simiyu aliandamana na kundi la wafuasi wa kanisa lake alipojiwasilisha katika afisi za mkuu wa polisi wa Bungoma Bw Kooli. Alikuwa ameagizwa kujiwasilisha kwa polisi kwa ajili ya mahojiano kuhusiana na kanisa lake.

Kufuatia agizo hilo, mchungaji huyo alikuwa ametoa ombi kwa polisi kutomtia mbaroni huku akibainisha kuwa hana makosa yoyote.

Akizungumza siku ya Jumatatu, Simiyu alisema hajafanya kosa lolote kufanya akamatwe, akiongeza kuwa anaeneza injili pekee.

“Najua hata kamanda wa polisi aliyeniita ni binadamu mwenye hekima. Ninaelewa anataka kuzungumza nami kuhusu masuala ya kanisa langu na jinsi linavyoendeshwa,” alisema.

"Labda wanasikia mambo ambayo hayapo kwa sababu nimekuwa kwa OCPD na OCS na sina shisa, ninahubiri injili tu."

Alisema akikamatwa watakuwa wanamhujumu tu kwa sababu ni wale wa upande mbaya wa sheria ndio wanaokamatwa.

Kooli alimwita kiongozi huyo wa kanisa la New Jerusalem kuhojiwa kuhusu mafundisho ya kidini yanayodaiwa kutiliwa shaka.