Mastaa wa soka walioachwa nje ya kikosi cha Ufaransa kwenda Qatar

Ufaransa wataelekea Qatar kutetea ubingwa wao bila baadhi ya wachezaji nguli walioshinda taji hilo Urusi 2018.

Muhtasari

• Mabingwa hao watetezi wa kandanda duniani wako Kundi D la michuano hiyo pamoja na Denmark, Tunisia na Australia.

Mastaa wa Ufaransa watakaokosa kushiriki kombe la dunia
Mastaa wa Ufaransa watakaokosa kushiriki kombe la dunia
Image: Instagram

Kocha Mkuu wa Ufaransa, Didier Deschamps amewaacha nje wachezaji kadhaa wakubwa baada ya kutaja kikosi chake cha wachezaji 25 kitakachoshiriki Kombe la Dunia. Paul Pogba na N'Golo Kante ni baadhi ya wachezaji bora ambao hawajajumuishwa kwenye kikosi, huku wachezaji hao wawili wa kiungo kwa sasa wakiwa majeruhi.

Wachezaji wengine nyota ambao hawakufuzu ni pamoja na fowadi wa Man United Anthony Martial na Ferland Mendy wa Real Madrid. Mabingwa hao watetezi wa kandanda duniani wako Kundi D la michuano hiyo pamoja na Denmark, Tunisia na Australia.

Licha ya kucheza nafasi muhimu katika ushindi wa Ufaransa wa Kombe la Dunia miaka minne iliyopita nchini Urusi, Pogba na Kante hawatacheza nafasi yoyote katika kampeni ya timu hiyo kutetea taji.

Pogba aliachwa nje kutokana na jeraha la goti ambalo limemfanya kukosa sehemu bora ya msimu mpya, huku Kante akiuguza jeraha la misuli ya paja.

Yafuatayo ni majina ya vinara walioachwa kwenye kikosi cha Ufaransa: Paul Pogba (Juventus), N'Golo Kante (Chelsea), Anthony Martial (Man United), Ferland Mendy (Real Madrid), Lucas Digne (Aston Villa), Wesley Fofana (Chelsea), Tanguy Ndombele ( Napoli), Boubacar Kamara (Aston Villa), na Theo Hernandez (AC Milan).

Licha ya kupata jeraha la musuli wa paja wiki kadhaa zilizopita, beki wa kati wa Manchester United, Raphael Verane anajihakikishia nafasi katika kikosi cha Ufaransa kitakachosafiri kuelekea Qatar kutetea ubingwa wao.

Hata hivyo, Ufaransa bado wanajivunia majina tajika kama vile kipa Hugo Lloris, Kylian Mbappe, William Saliba, Karim Benzema, Olivier Giroud, na Christopher Nkunku miongoni mwa wengine ambao wamejukumishwa kulitetea taji hilo.