Ivan Toney ateuliwa nahodha wa Brentford mechi yake ya kwanza baada ya marufuku miezi 8

Wachanganuzi wa spoti wanahisi hii ni njia moja ya Brentford kuonyesha kuwa wanamdhamini huku timu kubwa zikiwa zimemtolea kucha tayari kunasa saini yake.

Muhtasari

• Toney alifunga mabao 20 katika mechi 30 za ligi msimu uliopita kabla ya kupigwa marufuku na FA.

• Kurejea kwa fowadi huyo hakungeweza kuja kwa wakati mzuri zaidi klabu ikiwa katika nafasi ya 16

Ivan Toney
Ivan Toney
Image: Facebook

Kocha mkuu wa Brentford Thomas Frank amesema kuwa Ivan Toney atakuwa nahodha wa timu fowadi huyo atakaporejea kutoka kwa marufuku ya miezi minane dhidi ya Nottingham Forest kwenye Ligi ya Premia siku ya Jumamosi.

Toney alisimamishwa kujihusisha na soka na Shirikisho la Soka la Uingereza (FA) baada ya kushtakiwa kwa jumla ya ukiukaji 262 wa kanuni za kamari za shirikisho hilo.

Marufuku ya mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 27 hatimaye ilipunguzwa baada ya kugundulika kuwa mraibu wa kamari, na kumruhusu kufanya mazoezi na kucheza bila mashabiki mechi za kirafiki kwa Brentford B kujiandaa kurejea kwenye kikosi cha kwanza.

"Anapiga kelele kama mvulana wa miaka minane ambaye anataka kutoka na kucheza mchezo wake wa kwanza wa kandanda -- ni furaha tupu," meneja wa Brentford aliambia mkutano wa wanahabari.

"Ninatazama machoni mwa mchezaji ambaye anajituma sana na mwenye furaha kubwa. Nitaivunja sasa ataanza kesho, na pia ataiongoza timu kutoka kwenye handaki kama nahodha."

Toney alifunga mabao 20 katika mechi 30 za ligi msimu uliopita kabla ya kupigwa marufuku na FA.

Kurejea kwa fowadi huyo hakungeweza kuja kwa wakati mzuri zaidi klabu ikiwa katika nafasi ya 16, pointi tatu juu ya eneo la kushushwa daraja, na pointi moja nyuma ya Forest iliyo nafasi ya 15.

"Sio tu wiki hii, miaka mitatu na nusu iliyopita, yeye ni mhusika maalum kwa njia nyingi, ni mtu mzuri sana kuwa karibu nami, wafanyikazi, wachezaji, nguvu anayoleta, tabasamu, chanya kwenye uwanja wa mazoezi," Frank alisema.

"Akiwa uwanjani anataka kushinda, anataka kuisaidia timu, bila shaka ni ongezeko kubwa. Ni kama usajili mpya. Ni mshambuliaji wa pili bora kwa maoni yangu kwenye Ligi Kuu."

Wasiwasi mmoja kwa Frank ni kwamba kwa kuwa dirisha la usajili la Januari bado lipo wazi, Toney anaweza kuvutiwa na ofa ya pesa nyingi kutoka kwa Chelsea na Arsenal ambao wana nia ya kutaka kumnunua mchezaji huyo wa kimataifa wa Uingereza, kulingana na vyanzo vya ESPN.