EACC yadinda agizo la DPP kuchunguza madai ya uhamisho wa kura

EACC alipendekeza DPP kuelekeza Tume Huru ya Uchaguzi na mipaka (IEBC) kufanya uchunguzi huo.

Muhtasari

• Alhamisi DPP alituma barua kwa Mbarak akimtaka achunguze uhamishaji wa kura usio wa kawaida katika eneo bunge la Eldas huko Wajir na Balambala kaunti ya Garissa. 

Afisa mkuu mtendaji wa EACC Twalib Mbarak.
Afisa mkuu mtendaji wa EACC Twalib Mbarak.

Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) imekataa agizo la Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma Noordin Haji kuchunguza madai ya uhamisho wa wapigakura kinyume cha sheria. 

Haya ni kwa mujibu wa barua iliyoandikwa Ijumaa, Agosti 5, na Afisa mkuu mtendaji wa EACC Twalib Mbarak. Mbarak, hata hivyo, alipendekeza kuwa DPP anafaa kuelekeza Tume Huru ya Uchaguzi na mipaka (IEBC) kufanya uchunguzi huo. 

Alidokeza kuwa kesi au madai yoyote yanayohusiana na uchaguzi hayako chini ya mamlaka yake. 

"Tafadhali kumbuka kuwa madai ya usajili na uhamisho wa wapiga kura kinyume cha sheria hayako chini majukumu ya EACC na inapendekezwa kuwa IEBC ishughulikie suala hilo kwa mujibu wa mamlaka yao," barua ya Mbarak ilisema. 

Mnamo Alhamisi, Haji alituma barua kwa Mbarak akimtaka achunguze uhamishaji wa kura usio wa kawaida katika eneo bunge la Eldas huko Wajir na Balambala kaunti ya Garissa. 

"Naagiza kwamba uanzishe uchunguzi wa kina juu ya madai hayo na kisha uwasilishe faili ya uchunguzi wa matokeo ili kuchunguzwa na maelekezo zaidi," Haji alisema. 

Wafanyakazi watano wa IEBC wanadaiwa kuhusika.Wao ni pamoja na; Afisa wa ICT wa IEBC Garissa Adan Salah, ambaye ni afisa wa zamani wa ICT katika  eneo la Wajir, Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Ijara na aliyekuwa afisa mkuu wa uchaguzi eneo la Eldas Issack Muhumed na mwenzake wa Wajir Kaskazini Abdulahi Musa Mohammed. 

Wengine wanaohusishwa ni; aliyekuwa naibu afisa mkuu wa uchaguzi eneo la Balambala Mohammed Maow Abdi na Afisa mkuu wa uchaguzi wa Mbalambala Ali Noor Hussein.