Martin Wanyonyi: Albino wa Kwanza Kenya Kuchaguliwa bungeni

Wanyonyi ameandikisha historia ya kuwa mwanasiasa albino kuteuliwa Kenya kupitia kura ya debeni

Muhtasari

• Wanyonyi alipata jumla ya kura 12,864, akifuatiwa na Wanjala Iyaya wa DAP-K aliyepata kura 5,383. Wanyonyi alikuwa akiwania kwa chama cha FORD-K.

Mbunge mteule wa Webuye East, Martin Wanyonyi
Mbunge mteule wa Webuye East, Martin Wanyonyi
Image: Facebook

Martin Wanyonyi wa Ford Kenya amekuwa mtu wa kwanza mwenye ualbino kuchaguliwa kupitia kura nchini Kenya, baada ya kunyakua kiti cha Ubunge wa Webuye Mashariki.

Wanyonyi alipata jumla ya kura 12,864, akifuatiwa na Wanjala Iyaya wa DAP-K aliyepata kura 5,383. Wanyonyi alikuwa akiwania kwa chama cha FORD-K.

Akihutubia wanahabari baada ya kutangazwa mshindi, Wanyonyi aliwashukuru wakazi wa Webuye Mashariki kwa kumwamini, na kuongeza kuwa yuko tayari na amedhamiria kuwahudumia kulingana na matarajio yao.

“Uchaguzi huu ni wa kihistoria kwa sababu ni mara ya kwanza kwa mtu mwenye ualbino kuchaguliwa kupitia kura. Ninataka kuwahakikishia wakazi wa Webuye Mashariki kwamba nitatekeleza ahadi zangu,” alisema Wanyonyi.

Huyu anakuwa mlemavu wa Ngozi wa kwanza kabisa kuwahi kutokea na kushinda uchaguzi wa Kenya tangu uhuru wa miaka ya 60 ambapo wengi wamekuwa wakipendekezwa bungeni kuwakilisha makundi ya watu wenye mahitaji ya kipekee.

Mwanasiasa maarufu Isaac Mwaure ndiye maarufu nchini kwa kuwa zeruzeru anayewakilisha watu wenye ulemavu wa Ngozi bungeni ila hakuwahi kuteuliwa kupitia kura ya debe kama ambapo Wanyonyi ameandikisha historia, Mwaure amekuwa akipendekezwa na katika uchaguzi wa mchujo mwaka huu alishindwa katika mchujo wa UDA ambapo alinuia kuwa mbunge wa Ruiru.

Wakfu wa Colour Kwa Face (CKF) ambao ulianzishwa na mwanamuziki Nonini ili kuwatetea watu wenye ulemavu wa Ngozi nchini lilifurahia ushindi wa Wanyonyi na kumpongeza kwa kuingia kwenye vitabu vya historia kuwa albino wa kwanza kuwahi kuteuliwa kupitia kura.

“Hongera Mbunge Mteule Webuye Mashariki - Martin Wanyonyi,” Wakfu wa CKF uliandika kupitia Instagram yao.