Tuko tayari kukabiliana nanyi mahakamani- Nelson Havi awaambia wanaAzimio

Raila ameapa kuenda mahakamani kupinga matokeo yaliyotangazwa na Chebukati Jumatatu.

Muhtasari

•Havi alisema kwamba wako tayari kuwashughulikia iwapo watawasilisha ombi la kupinga matokeo ya urais katika Mahakama ya Juu.

•Mgombea urais wa Azimio Raila Odinga tayari ameapa kuenda mahakamani kupinga matokeo yaliyoachiliwa na Chebukati.

Mwenyekiti wa LSK Nelson Havi

Wakili Nelson Havi ameambia Muungano wa Azimio la Umoja One Kenya kwamba wako tayari kuwashughulikia iwapo watawasilisha ombi la kupinga matokeo ya urais katika Mahakama ya Juu.

Havi, ambaye alishindana katika kinyang’anyiro cha ubunge wa Westlands kwa tiketi ya UDA lakini akashindwa na Tim Wanyonyi wa ODM alipuuza suala hilo iwapo lingewasilishwa.

"Tuko tayari kukabiliana katika Mahakama ya Juu. Kwa hakika, tutatumia hoja zao wenyewe kuhusu ‘quorum’ ya IEBC na uamuzi wa Mahakama kuhusu kesi hiyo hiyo katika kesi ya BBI," Havi alisema.

"Itakuwa vita fupi zaidi iliyopiganwa katika Mahakama ya Apex."

Mgombea urais wa Azimio Raila Odinga tayari ameapa kuenda mahakamani kupinga matokeo yaliyoachiliwa na Chebukati.

Akizungumza katika ukumbi wa Bomas siku ya Jumanne,Raila alisema kuwa ana ushahidi wa kutosha dhidi ya matokeo hayo na kuashiria imani yake kuwa yatabatilishwa.

"Hatutakubali mtu mmoja ajaribu kuleta vurugu katika taifa letu na kubadilisha yale ambayo Wakenya wameamua kama watu moja. Wakenya hawatakubali, hatutakuli. Tutazidi kutetea nchi yetu na katiba letu kama Wakenya ili Kenya iweze kuenda mbele,"

Mgombea urais huyo wa Azimio alishindwa katika kinyang’anyiro cha Agosti 9 na mpinzani wake wa muda mrefu, Naibu Rais William Ruto.

Mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati Jumatatu alimtangaza Ruto kuwa Rais mteule baada ya kupata kura 7,176,141 (asilimia 50.49) dhidi ya kura 6,942,930 za Raila (asilimia 48.85).