Gavana mteule Kawira Mwangaza ajiunga rasmi na Kenya Kwanza

Kawira amedokeza kuwa aliichukua hatua ya kujiunga na Ruto katika lengo la kufanikisha maendeleo Meru.

Muhtasari

•Kawira alijiunga rasmi na Kenya Kwanza Ijumaa asubuhi na kupokewa na Ruto katika ofisi yake ya Karen, Nairobi.

•Kawira amedokeza kuwa alichukua hatua ya kujiunga na Ruto katika lengo la kufanikisha maendeleo huko Meru.

nje ya ofisi za naibu rais katika mtaa wa Karen, Nairobi mnamo Agosti 19, 2022.
Gavana mteule wa Meru Kawira Mwangaza na rais mteule William Ruto nje ya ofisi za naibu rais katika mtaa wa Karen, Nairobi mnamo Agosti 19, 2022.
Image: FACEBOOK// KAWIRA MWANGAZA

Gavana mteule wa kaunti ya Meru Kawira Mwangaza amejiunga na kambi ya Kenya Kwanza inayoongozwa na rais mteule William Ruto.

Kawira alijiunga rasmi na Kenya Kwanza Ijumaa asubuhi na kupokewa na Ruto katika ofisi yake ya Karen, Nairobi.

"Asante Gavana Mteule wa Kaunti ya Meru Kawira Mwangaza kwa kuchagua kufanya kazi na Kenya Kwanza ili kusukuma mbele Meru na Kenya, Karen, Kaunti ya Nairobi," Ruto alisema kupitia Facebook.

Aliambatanisha ujumbe huo na picha inayoonyesha akimsalimia gavana huyo mteule nje ya ofisi yake.

Kawira alinyakua kiti cha ugavana wa Meru kama mgombea huru. Alipata kura 209,148 huku Mithika Linturi wa UDA akiibuka wa pili kwa kura 183,859.

Gavana anayeondoka Kiraitu Murungi alichukua nafasi ya tatu kwa kura 110,814

Kawira amedokeza kuwa alichukua hatua ya kujiunga na Ruto katika lengo la kufanikisha maendeleo huko Meru.

"Rais Mteule Akutana na Gavana Mteule. Kufanya kazi kuelekea maendeleo endelevu," Gavana huyo mteule alisema kwenye Facebook.

Akizungumza baada ya kupokea cheti cha ushindi Ijumaa wiki jana, Kawira alimshukuru Mungu, mumewe Murega Baichu, naibu wake Isaac Mutuma na jamii ya Wameru kwa kuamini uongozi wake wa LL.

"Ninawaahidi, Meru itakuwa kaunti bora zaidi. Kutakuwa na miradi ya maendeleo endelevu. Tunaanza kufanya kazi sasa hivi na ninaamini Meru itakuwa bora zaidi nchini Kenya. Nitawaunganisha Wameru wote licha ya makabila yao madogo," Kawira alisema.

Pia aliwataka wabunge wote wa Meru kufanya kazi pamoja kwa ajili ya ukuaji na ustawi wa Kaunti hiyo.