Hatuwezi kuchukua umiliki wa matokeo yatakayotangazwa! Makamisha 4 wapinga matokeo

Makamishna hao walisema kuwa hawakuridhishwa na jinsi hatua ya mwisho ya uchaguzi ilivyoendelezwa.

Muhtasari

•Makamishna wanne wa tume ya uchaguzi na mipaka wamejitenga na matokeo ya uchaguzi wa urais yanayotarajia kuachiliwa.

•Cherera alibainisha kuwa watu ambao hawataridhishwa na matokeo wapo huru kuelekea mahakamani.

Makamishna Juliana Cherera, Francis Wanderi, Irene Masit na Justus Nyangaya.
Makamishna Juliana Cherera, Francis Wanderi, Irene Masit na Justus Nyangaya.
Image: FREDRICK OMONDI

Baadhi ya makamishna wa tume ya uchaguzi na mipaka wamejitenga na matokeo ya uchaguzi wa urais yanayotarajia kuachiliwa.

Makamishna wanne wakiongozwa na naibu mwenyekiti  wa tume Juliana Cherera  walifanya mkutano na waandishi wa habari katika Hoteli ya Serena na kueleza kuwa hawakuridhishwa na jinsi hatua ya mwisho ya uchaguzi ilivyoendelezwa.

"Tumefanya uchaguzi wa 2022 kwa njia bora zaidi. Tumehakikisha kuwa tumeboresha viwango.  Tumefanya kazi nzuri lakini baadhi ya mambo yanahitaji kuwekwa wazi.Tupo hapa kwa sababu ya hali ya kutoeleweka ambayo hatua ya mwisho ya uchaguzi mkuu huu. Hatuwezi kuchukua umiliki wa matokeo ambayo yanaenda kutangazwa," Cherera alisema.

Kamishna huyo alibainisha kuwa watu ambao hawataridhishwa na matokeo wapo huru kuelekea mahakamani.

Cherera alikuwa ameandamana na Francis Wanderi, Irene Masit na Justus Nyangaya. Alisema watatoa taarifa ya kina baadaye.

Makamishna wote waliajiriwa mwaka jana.

Wakati wanahabari bado wakiendelea, machafuko yalizuka katika ukumbi wa Bomas of Kenya, kituo cha kitaifa cha kujumlisha matokeo ambapo tangazo la matokeo lilitarajiwa kutolewa na mwenyekiti Wafula Chebukati.

Zikiwa zimesalia dakika chache hadi saa kumi na mbili jioni, haikufahamika kama mwenyekiti bado angetangaza matokeo au la.

Hapo awali Chebukati alikuwa amewahakikishia Wakenya kwamba hatatangaza mshindi wa kinyang'anyiro cha urais usiku.