"Mimi na Ross ni familia!" Hamisa Mobetto afunguka kuhusu uhusiano wake na Rick Ross

Muhtasari

•Mpenzi huyo wa zamani wa Diamond Platnumz alisema mkutano wao wa kwanza ulikuwa mzuri huku akifichua walikuwa wanawasiliana mara kwa mara kwa simu hata kabla wakutane Dubai.

•Mobetto hakukiri kuwa na mahusiano ya kimapenzi na rapa huyo wala kukana huku akiahidi kufahamisha watu hivi karibuni iwapo kuna chochote cha ziada kati yao.

•Alipuuzilia mbali kuwa alionekana akibusu Ross kwenye video huku akidai maneno matamu ya kimapenzi ambayo rapa huyo alisikika akimuita walipokuwa kwenye klabu hayakumaanisha chochote.

Image: INSTAGRAM// HAMISA MOBETTO

Huku maoni na hisia mbalimbali zikiendelea kutolewa kufuatia video na picha zilizochapishwa wiki iliyopita, mwigizaji na mwanamuziki Hamisa Mobetto ameeleza uhusiano wake na nyota wa Hiphop Rick Ross.

Alipokuwa anahutubia wanahabari siku ya Jumamosi punde baada ya kutua katika uwanja wa ndege wa Julius Kabarage Nyerere kutoka Dubai, Mobetto aliweka wazi kuwa mkutano wake na Rick Ross wa wiki iliyopita ndio ulikuwa wa kwanza kabisa.

Mpenzi huyo wa zamani wa Diamond Platnumz alisema mkutano wao wa kwanza ulikuwa mzuri huku akifichua walikuwa wanawasiliana mara kwa mara kwa simu hata kabla wakutane Dubai.

"Ilikuwa mara yangu ya kwanza kukutana naye. Yeye ni mzuri sana. Kila kitu nilichokuwa nahisi, yuko hivo. Nilikuwa naongea naye kwa hivyo sikupata shida tulipokutana kwa sababu nilishazoea kuongea naye. Yeye ana roho ya ajabu, yeye ni muungwana" Mobetto alisema.

Mwigizaji huyo alitaja uhusiano wake na Rick Ross kama wa 'kifamilia' kwani wamekuwa wakifanya kazi pamoja kwa muda.

Mobetto hakukiri uwepo wa mahusiano ya kimapenzi kati yake na rapa huyo wala kukana huku akiahidi kufahamisha watu hivi karibuni iwapo kuna chochote cha ziada kati yao.

"Mimi na Ross ni familia. Saa hii tumekuwa familia, hayo ndiyo naweza kusema. Zaidi ya hayo mimi nimekuwa balozi wa Belaire hapa Tanzania. Huwa tunafanya kazi pamoja... Kama kutakuwa na kitu chochote kitatokea mtajua tu" Alisema Mobetto.

Mobetto alisema ziara yake ya Dubai ilikuwa ya kikazi tu ikiwemo kujadiliana na Rick Ross ambaye ni mshirika wake kazini.

Alisema rapa huyo mzaliwa wa Marekani ana mapenzi makubwa kwa Tanzania na hata ana mpango wa kuwekeza Bongo hivi karibuni.

"Nilienda Dubai kwenye kazi na biashara zangu. Pia Rick Ross amepanga kuja kuwekeza. Ana mipango ya kufanya Tanzania iwe makao yake ya pili. Anasifia sana Tanzania, amemtaja hata rais wetu Bi. Samia. Ni mtu ambaye ana nia njema na Tanzania nami ni Mtanzania ambaye anafanya kazi naye. Iwapo kutakuwa na kitu kingine cha ziada basi mtaona. Anakuja Tanzania hivi karibuni, sijui tarehe ipi lakini" Mobetto alisema.

Mwigizaji huyo alipuuzilia mbali kuwa alionekana akibusu Ross kwenye video huku akidai maneno matamu ya kimapenzi ambayo rapa huyo alisikika akimuita walipokuwa kwenye klabu hayakumaanisha chochote.