Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan alitangaza kuwa serikali yake itagharamia matibabu ya mwanamuziki huyu sifika.
Mwanamuziki na mwanasiasa mashuhuri kutoka Tanzania Joseph Haule almaarufu Profesa Jay amekuwa hospitalini kwa kipindi cha takriban wiki nne akiwa katika hali mahututi.
Siku ya Jumamosi rais Samia Suluhu Hassan alitangaza kuwa serikali yake itagharamia gharama ya matibabu ya mwanamuziki huyu sifika ambayo imeendelea kupanda kila siku.
Haya yanajiri baada ya kufichuliwa kwamba afya ya msanii huyo sio shwari na familia yake kwa ushirikiano na baadhi ya watu mashuhuri kupanga jinsi ya kuomba michango ya kufanikisha matubabu yake.
Jumamosi iliyopita familia ya Profesa Jay ikishirikiana na kituo kimoja cha habari nchini humo waliandalia mbunge huyo wa zamani wa Mikumi hafla maalum ya maombi.
Maombi hayo yalihudhuriwa na watu wa tabaka mbalimbali na kwa pamoja wakamtakia mwamuziki huyo afueni ya haraka.
Habari za kuugua kwa Profesa Jay zilisambaa mitandaoni wiki jana na maelfu ya wanamitandao wamekuwa wakimwandika jumbe za afueni ya haraka.