"Alikuwa ananipiga sana!" Baba mtoto wa Amber Lulu afunguka masaibu ya ndoa yao iliyovunjika

Botion alisema alishindwa kulalamika kuhusu kupigwa na kipusa huyo kwa kuwa aliogopa kupata aibu.

Muhtasari

•Botion aliweka wazi kuwa sio yeye pekee aliyekuwa akimpiga Amber Lulu, bali pia mzazi huyo mwenzake alimpiga mara kwa mara.

•Botion alisema hakuwahi kuwaeleza watu wake wa karibu kuhusu vipigo alivyokumbana navyo wakati wa ndoa yao. 

Mr Botion na Amber Lulu
Image: HISANI

Mzazi mwenza wa mwanasosholaiti Amber Lulu, mwimbaji Emba Botion amefunguka kuhusu masaibu ya ndoa yao iliyovunjika.

Akizungumza kwenye mahojiano na Wasafi Media, Bw Botion alifichua kwamba ndoa yao ilikumbwa na mapigano kila mara.

Aliweka wazi kuwa sio yeye pekee aliyekuwa akimpiga Amber Lulu, bali pia mzazi huyo mwenzake alimpiga mara kwa mara.

"Na yeye pia alikuwa ananipiga. Yeye mwenyewe alikuwa ananipiga sana," Botion alisema.

Mwanamuziki huyo alisema kuwa alishindwa kulalamika kuhusu kupigwa na mwanasosholaiti huyo kwa kuwa aliogopa kupata aibu. Aidha, alibainisha kuwa mwili wake haukuwa unaonyesha dalili za kupigwa, kama vile wa mwenzake Amber Lulu, kwa kuwa ngozi zao ni tofauti, yake ikiwa ngumu zaidi.

"Ngozi yake haipoi hivo, ata ukimpiga kidogo inakuwa pevu. Ata yeye alikuwa ananipiga, ni vile tu sikuja kusema ananipiga, hiyo aibu," alisema.

Botion alisema hakuwahi kuwaeleza watu wake wa karibu kuhusu vipigo alivyokumbana navyo wakati wa ndoa yao. Alisema kwamba angeiruhusu familia zao zisaidie kushughulikia masuala yao hadi watakapotengana.

Aliendelea kudokeza kuwa licha ya kuachana, bado wako katika maelewano mazuri na hata wanashirikiana katika malezi.

"Mimi sio tajiri, sina mihela lakini kinachopatikana tunasapoti... tunaongea freshi tu, hamna tatizo lolote," alisema.

Alibainisha kuwa baada ya mahusiano yao kugonga mwamba walibaki washikaji wakubwa kama jinsi ilivyokuwa awali.

Mapema mwaka huu, Amber Lulu aliibua madai mazito dhidi ya mzazi huyo mwenzake huku akidai alikuwa akimdhulumu.

Mwanamuziki huyo  alidai kuwa Botion hata aliapa kumuua ila alistahimili tu kutoka na upendo wake kwa mtoto wao.

"Daa nimekuwa mtu wa kuhangaika na kuteseka pasiposababu ya msingi mapenzi niliyo nayo kwa mtoto wangu na uchungu na uvumilivu Mungu pekee ndio anajua kuna muda najitoa kufanya chochote kwa ajili ya mwanangu," alisema kwenye Instagram huku akionyesha alama za kupigwa kwenye mwili wake.

"Nilizaa kwa mapenzi na mapenzi ya Mungu ila nachofanyiwa kama sina haki kuna muda natamani kumkumbatia mwanangu nishinde nae nashindwa coz nisipo hangaika mwanangu atakula nn??Nyumba nalipa na nn??

Leo napigwa kama mbwa,kisa kumwangaikia mwanangu naumia sa ivi mtu ananitishia kuniua Mungu," Lulu alifichua kwenye ukurasa wake wa Instagram.

Mpenzi huyo wa zamani wa rapa wa Kenya Jackson Makini almaarufu Prezzo aliongeza kuwa alichukizwa sana na jinsi mwili wake ulivyoonekana vibaya kutokana na mapigo aliyopata kutoka kwa mumewe.

"Mpaka naogopa kurudi nyumbani kwangu mtoto wangu namuita hotel kuangalia mwili wangu kama daaah."