"Maisha yamekuwa magumu!" Mwanamuziki wa Sailors Gang afunguka masaibu yaliyowakumba

Muhtasari

•Juma amesema kwa sasa maisha yamekuwa magumu licha ya umaarufu mkubwa waliopata miaka kadhaa iliyopita.

•Juma amefichua kuwa masuala mbalimbali hayawaruhusu kutengeneza muziki pamoja kwa sasa.

Mwanamuziki Cocos Juma wa Sailors Gang
Mwanamuziki Cocos Juma wa Sailors Gang
Image: INSTAGRAM// COCOS JUMA

Mwanamuziki wa bendi ya Sailors Gang Cocos Juma amelalamikia hali ya maisha yake tangu alipojitosa kwenye usanii.

Akizungumza katika Plug TV, Juma alisema kwa sasa maisha yamekuwa magumu licha ya umaarufu mkubwa waliopata miaka kadhaa iliyopita.

Juma aliwezwa na hisia na kudondokwa na machozi  alipokuwa anasimulia yaliyompata. Alidai kuwa masaibu yalianza kumwandama yeye na wanabendi wenzake tangu waliposaini mkataba na lebo ya muziki.

"Maisha imekuwa ngumu. Tangu niingie kwenye usanii maisha yamekuwa magumu. Nashindwa kwani vijana tulikosea wapi. Vijana wakija kujiinua wanapigwa, si wasimamizi, si lebo. Sasa tunaimba tofauti, hatuwezi kuimba kama timu," Alisema.

Mwanamuziki huyo alilalamika kuwa lebo nyingi zimekuwa zikiwahadaa wasanii chipukizi ndiposa wengi wao wameshindwa kujiendeleza.

"Usanii una pesa lakini kuna watu ambao wanazikula. Hapa Kenya ufisadi ndio uko kila mahali," Alisema.

Licha ya masaibu yaliyowakumba, Juma hata hivyo amesisitiza kuwa kundi lao la Sailors Gang bado lipo imara pamoja. Hata hivyo amefichua kuwa masuala mbalimbali hayawaruhusu kutengeneza muziki pamoja kwa sasa.

Juma pia alidai kuwa wasanii wengi chipukizi wanajitosa kwenye uraibu wa mihadarati kutokana na machungu wanayopitia wakijaribu kufanya sanaa yao.

"Si kutaka kwao. Wengi wanapitia kwenye machungu. Wengine wao wanalea. Wengi wana msongo wa mawazo," Alisema.

Msanii huyo amefichua kuwa kwa sasa anajihusisha na kazi ya kutengeneza nywele za dreadlocks baada ya taaluma ya muziki kulememazwa.

Aidha ametoa ombi kwa serikali kutengeneza sheria ambazo zitawezesha wasanii kupata mafanikio kutokana na muziki wao.