Maafisa wawili wa polisi wakamatwa Narok wakiwa na karatasi za kupiga kura zenye alama

Vifaa hivyo vilikuwa bado vikisafirishwa kulingana na maafisa wa IEBC katika eneo hilo

Muhtasari

•Maafisa ambao walikuwa wametiwa mbaroni tangu wakati huo walinaswa na karatasi hizo katika Kituo cha Petroli cha Shell huko Kilgoris baada ya wananchi kutoa tahadhari.

•Walitambuliwa kama Michael Cheptoo, Sajenti na Daniel Chepkwony, afisa wa polisi.

Image: Maktaba

Polisi huko Kilgoris wanawashikilia watu watatu, miongoni mwao maafisa wawili wa polisi, kwa madai ya kusafirisha karatasi za kupigia kura ambazo tayari zilikuwa zimewekwa alama za kupiga kura na vifaa vingine vya uchaguzi.

Katika taarifa, Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Narok, Kizito Mutoro alisema washukiwa hao walikamatwa saa kumi na mbili na nusu jioni ya Jumatatu baada ya wananchi kulifuata gari hilo na kudokeza taarifa hizo kwa vyombo vya dola.

"Polisi walipokea simu ya dokezo kutoka kwa wananchi ambao walisema wamekamata karatasi za kupigia kura zilizowekwa alama kwenye kituo cha mafuta. Polisi walikimbia eneo la tukio ambapo walikuta gari aina ya Toyota Sienta likiwa limebeba vifaa vya uchaguzi chini ya askari polisi wawili," Kamanda wa polisi Mutoro alisema.

Alisema kuwa washukiwa walikuwa wameenda kwenye kituo cha petroli katika mji wa Kilgoris ili kujaza gari lao. Alisema washukiwa hao wanashikiliwa katika Kituo cha Polisi cha Kilgoris.

Miongoni mwa nyenzo zilizopatikana ni pamoja na daftari moja la wapiga kura katika Gereza la Kilgoris, vijitabu viwili vya matokeo ya uchaguzi, pakiti 12 za karatasi za kupigia kura za urais na nne za 35c.

"Sanduku moja la kura za urais liliharibiwa na wananchi. Msimamizi wa kura katika eneo bunge la Transmara magharibi alithibitisha kuwa vifaa vilivyonaswa ni mali ya IEBC," akaongeza.

Visa hivi vinajiri huku taifa likitarajiwa kuelekea debeni kuwachagua viongozi wao kwa kipindi kingine cha miaka mitano ijayo.