Magavana wanaoondoka waaga wafuasi wao.

Magavana wanaoondoka ambao muhula wao wa pili umekamilika wameanza kuwaaga watu wao

Muhtasari

•Magavana wengine wanaoondoka ni Ali Roba (Mandera), Kivutha Kibwana (Makueni), Okoth Obado (Migori), Cyprian Awiti (Homa Bay), James Ongwae (Kisii) na Hassan Joho (Mombasa) miongoni mwa wengine.

Magavana
Magavana
Image: Handout

Magavana wanaoondoka ambao muhula wao wa pili umekamilika wameanza kuwaaga watu wao wanapoondoka afisini, kabla ya hafla ya kesho ya kuwaapisha Magavana wapya waliochaguliwa.

Gavana anayeondoka wa Machakos Alfred Mutua kupitia video iliyochapishwa katika akaunti yake ya Twitter mnamo Jumatano alichukua muda kuwashukuru wakazi wa Machakos kwa kumpa nafasi ya kuwatumikia kwa mihula miwili.

Mutua pia alisema kuwa wakati alipotangazwa kama gavana bora, alijawa na furaha sana, haya yote ni kwa ajili ya nafasi wakaazi wa Machakosa walimpea kuwaongoza kama gavana.

Mutua alitawazwa kuwa gavana bora zaidi barani mnamo Disemba 2021, na kampuni ya vyombo vya habari yenye makao yake nchini Nigeria,'My Media Africa', ambayo iliwaorodhesha viongozi wa Afrika kutokana na mafanikio mbalimbali katika uongozi.

Mwenzake wa Kilifi Amason Kingi Jumatatu aliandaa chakula cha mchana na wafanyakazi wake katika afisi yake mjini Kilifi.

Kingi alijigamba kuwa ameweka msingi imara wa maendeleo, mabadiliko ya maisha, utoaji wa huduma kwa Wananchi na kuweka mazingira mazuri ya kufanya biashara.

“Leo, tunaondoka ofisini tukijua kwamba tulitimiza wajibu wetu na kutimiza ahadi tulizotoa kwa wapiga kura wa Kilifi wakati wa uchaguzi mkuu wa 2013 na 2017. Mungu Ibariki Kaunti ya Kilifi,” Amason Kingi alisema.

Magavana wengine wanaoondoka ni Ali Roba (Mandera), Kivutha Kibwana (Makueni), Okoth Obado (Migori), Cyprian Awiti (Homa Bay), James Ongwae (Kisii) na Hassan Joho (Mombasa) miongoni mwa wengine.