Wajackoyah awashukuru Githu Muigai na Orengo kwa kufanikisha safari yake kuwa wakili

Wajackoyah aliwania urais katika uchaguzi wa Agosti 9 na kumaliza wa tatu nyuma ya Odinga na Ruto.

Muhtasari

• Wajackoyah alifika katika mahakama ya upeo akitaka kujumuishwa katika kesi ya kupinga matokeo ila ombi lake likakataliwa.

Wakili msomi aliyekuwa mgombea wa urais akiwapongeza Githu Muigai na James Orengo kwa kumfanya kuwa mwanasheria
GEORGE WAJACKOYAH Wakili msomi aliyekuwa mgombea wa urais akiwapongeza Githu Muigai na James Orengo kwa kumfanya kuwa mwanasheria
Image: MAKTABA

Jumanne mahakama ya upeo iliandaa kikao cha utangulizi wa kusikiliza kesi ya kupinga matokeo ya urais ambapo jopo la majaji saba lilipata nafasi ya kusikiliza mawakili na wanasheria mbali mbali wakijitambulisha na kujieleza pande watakazoziwakilisha katika kesi hiyo.

Aliyekuwa mgombea urais katika uchaguzi huo ambao unapingwa mahakamani, wakili msomi Profesa George Wajackoyah alikuwa miongoni mwa wanasheria ambao walifika katika majengo ya mahakama ya upeo akitaka kujumuishwa katika kusikilizwa kwa kesi hiyo kama rafiki wa mahakama, ombi ambalo jopo la majaji lilikataa vikali kwa kigezo kwamba hakuwasilisha ombi la kutaka kubatilishwa kwa matokeo hayo ambayo alikuwa mmoja wa wagombea.

Baada ya ombi lake kukataliwa, Wajackoyah alichukua fursa hiyo kuwamiminia sifa aliyekuwa mwanasheria mkuu wa serikali Githu Muigai pamoja na wakili ambaye pia anajiongeza kama gavana wa Siaya, James Orengo kwa kusema kwamba wawili hao walikuwa na mchango mkubwa sana katika safari yake ya kufanikiwa kweney kitivo cha uanasheria.

“Ningependa kuwashukuru wale ambao wako hapa, haswa Githu Muigai na James Orengo kwa kufanikiwa zaidi kunifanya mtu ambaye niko leo hii na mhitimu mwenzangu jaji mkuu, ninasema kwamba tafadhali acha tuangalie zaidi ya kioo kwamba haki inaonekana kutendeka. Kuzungumza juu ya haki, nahitaji haki, na haki huanza katika chumba hiki," alisema wakili huyo msomi aliyefahamika zaidi kwa kufagilia ukulima wa bangi iwapo angechaguliwa kama rais wa tano wa Kenya.

Katika uchaguzi wa Agosti 9 mwaka huu, Wajackoyah alikuwa akiwania kama rais kupitia chama chake cha Roots pamoja na mgombea mwenza wake Justina Wamae ambae wamekuwa wakitofautiana pakubwa tangu kukamilika kwa uchaguzi huo huku duru zikiarifu kwamba tayari Wamae ameng’olewa kutoka chama hicho cha mizizi.

Kulingana na matokeo yaliyotangazwa na tume hutu ya uchaguzi na mipaka IEBC, Wajackoyah aliibuka wa tatu nyuma ya Raila Odinga wa Azimio aliyeibuka wa pili naye William Ruto wa UDA akiimaliza na medali ya dhahabu katika kipute hicho. David Mwaure wa Agano alikuwa wa mwisho nyuma ya Wajackoyah.