Bahati amhakikishia Mungu kuwa bado hajabadilika

Bahati amemwambia Mungu kuwa bado ameshikilia ahadi kuwa hatawahi muacha ambayo alimpatia alipokuwa anapokea tuzo la Groove

Muhtasari

•Amesema kuwa kuna watu wengi ambao wamekuwa wakimtumia video moja ya kikejeli ambayo ilirekodiwa akipokea tuzo la wimbo bora wa injili kwenye hafla ya Goove Awards 2015.

•Nyimbo za Bahati za hivi karibuni zimeibua gumzo kubwa haswa mitandaoni huku wengi wakidai kuwa mwanamuziki huyo amegura injili. Hata hivyo, Bahati amejitetea na kusema kuwa  yeye ni yule yule na hajabadilika.

Bahati
Bahati
Image: Instagram

Mwanamuziki Kevin Bahati almaarufu kama mtoto wa mama amelalamikia watu ambao wanamkashifu kwa kubadilisha mtindo wa muziki.

Amesema kuwa kuna watu wengi ambao wamekuwa wakimtumia video moja ya kikejeli ambayo ilirekodiwa akipokea tuzo la wimbo bora wa injili kwenye hafla ya Goove Awards 2015.

Msanii huyo ambaye anavuma sana kwa sasa baada ya kuzindua albamu 'Love like this'  yenye nyimbo kumi za mapenzi amesema kuwa bado hajabadilika.

Kupitia ujumbe alioandika kwenye mtandao wa Instagram, Bahati amehakikishia Mungu kuwa bado ameshikilia ahadi kuwa hatawahi muacha  ambayo alimpatia alipokuwa anapokea tuzo la Groove.

"Naapa mbele ya dunia, Mungu sitawahi kuacha" Bahati alisema kwa wakati ule.

Nyimbo za Bahati za hivi karibuni zimeibua gumzo kubwa haswa mitandaoni huku wengi wakidai kuwa mwanamuziki huyo amegura injili.

Hata hivyo, Bahati amejitetea na kusema kuwa  yeye ni yule yule na hajabadilika.

"Nimeona watu wengi wakinitumia na kunitaja  kwenye video hii (iliyoambatana na ujumbe wake). Lakini Mungu wajua roho yangu na wajua kuwa huyu bado ni mimi. Haya bado ni maneno yangu na wajua sijawahibadilika. Endelea kunishika mkono ninapopeleka muziki wa Kenya kote duniani" Bahati aliandika.

Kwa sasa mwanamuziki huyo yumo nchini Tanzania kurekodi video ya wimbo mmoja kwenye albamu yake ambao alishirisha mwanamuziki tajika wa bongo, Rayvanny. Bahati aliandamana na mpenzi wake, Diana Marua.