SIASA ZA JUJA

Kuria kupimana nguvu na rais Kenyatta Juja

Kuria anatazamia kupima ushawishi wake dhidi ya rais Uhuru Kenyatta kwenye uchaguzi mdogo eneo bunge la Juja

Muhtasari

•Kuria amesimamisha mgombeaji kupitia chama chake cha PEP

•Susan Njeri na George Koimburi ndio farasi wakuu kwenye uchaguzi huo

Mbunge wa Gatundu na naibu rais
Mbunge wa Gatundu na naibu rais
Image: File

Tarehe kumi na nane mwezi wa Mei ni tarehe muhimu sana kwa waakazi wa Juja kwani ndiyo tarehe rasmi ya uchaguzi wa kubaini nani atakayekuwa mbunge wa eneo hilo.

Ni kwenye uchaguzi huo bado ambako Mbunge wa Gatundu Kusini na ambaye ni kiongozi wa chama cha People's Empowerment Party(PEP) , Moses Kuria anatazamia kukabiliana na kupima ushawishi wake katika eneo la Kiambu dhidi ya rais Uhuru Kenyatta

Farasi wawili wakuu wanaoonekana kuwa na ushawishi mkubwa katika eneo bunge hilo ni ikiwemo mgombea kiti na tikiti ya Jubilee, Susan Njeri na George Koimburi wa chama chake Moses Kuria.

Uchaguzi huo mdogo ulialika wagombea kiti 13 huku mmoja wao kwa jina John Njoroge akitangaza kujiondoa siku moja tu kabla ya uchaguzi. Njoroge ambaye alikuwa anagombea kwa tikiti binafsi alitangaza kuwa angemuunga mkono Koimburi.

Kiti hicho kiliachwa wazi baada ya aliyekuwa mbunge, Francis Waititu 'Wakapee' kufariki mwezini Februari. Mjane wake, Susan Njeri, aliweza kuteuliwa kugombea kiti kile na tikiti ya Jubilee.

Tangu salamu za 'Handshake' kati ya Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa ODM Raila Odinga, kumekuwa na mgawanyiko mkubwa kwenye chama tawala cha Jubilee jambo ambalo limemfanya mbunge Moses Kuria kutokuwa katika hali ya maelewano na rais ambaye pia ni kiongozi wa Jubilee.

Kuria ameoneka kumpinga sana rais hadharani na pia kwenye mtandao. Anajihusisha na mrengo unaomuunga mkono naibu rais William Ruto almaruufu kama Tangatanga. Ingawa Kuria aliingia bungeni kwa tikiti ya Jubilee, amesita kabisa kujihusisha na chama hicho tena.

Kwenye uchaguzi huo, rais Kenyatta anamuunga mkono Susan Njeri na kwa upande wake Kuria anamuunga mkono Koimburi.Koimburi pia anaungwa mkono na chama cha United Democratic Party (UDA) kinachohusishwa na Ruto.

Wafuasi wa naibu rais wakekuwa makimpigia debe Koimburi huku wafuasi wa rais wakimpigia debe mjane wake Waititu.Matokeo ya uchaguzi huo yatakuwa na umuhimu mkubwa kwa rais Kenyatta na Kuria. Wawili hao watakuwa wakipima ushawishi wao katika kaunti ya Kiambu.