Mwanamke wa miaka 59 auawa na umeme akiwa shambani kwake Homabay

Jane Opala 59, alikuwa anapanda mahindi kwenye shamba lake wakati msiba huo ulitokea.

Muhtasari

•Alipokuwa anathibitisha tukio hilo, naibu chifu wa eneo hilo Bw Duncan Oketch alisema kuwa marehemu aliaga baada ya kugusa waya wa umeme ambao ulikuwa unasambaza stima kiharamu kwa nyumba zilizo karibu na shamba lake.

kenya power employees on powerline
kenya power employees on powerline

Habari na Faith Matete

Hali ya majonzi imetanda katika kijiji cha Arunda kaunti ya Homabay baada ya mwanamke mmoja kuuawa na nguvu za umeme akiwa shambani kwake.

Jane Opala 59, alikuwa anapanda mahindi kwenye shamba lake  wakati msiba huo ulitokea.

Opala alishika waya wa umeme akijaribu kuuondoa kwa njia ili aweze kupanda  bila kufahamu ulikuwa na stima na akafariki papo hapo.

Alipokuwa anathibitisha tukio hilo, naibu chifu wa eneo hilo Bw Duncan Oketch alisema kuwa marehemu aliaga baada ya kugusa waya wa umeme ambao ulikuwa unasambaza stima kiharamu kwa nyumba zilizo karibu na shamba lake.

Bw Oketch aliita Kenya Power kufanya msako katika eneo hilo ili kuwanasa wale ambao wameweka stima kwa manyumba zao kiharamu.

Raia walionywa dhidi ya kujihusisha na tabia hiyo kwani inasababisha maafa na ni ukiukaji wa sheria ambapo mtu anaweza kukamatwa na kushtakiwa.

Mwili wa marehemu ulipelekwa katika mochari ya Homabay huku polisi wakianza msako wa kuwinda ambao wanasambaza nguvu za umeme kiharamu.