Covid-19: Watu 7 waaga dunia huku 685 wakiambukizwa

Muhtasari
  • Watu 685 wapatikana na virusi vya corona na kufikisha idadi jumla ya 44,881
  • Watu 28 wamo katika chumba cha wagonjwa mahututi kufuatia maambukizi ya corona
  • Idadi ya maambukizi imeongezeka marudufu katika siku za hivi majuzi 
Mutahi Kagwe
Waziri wa Afya Mutahi Kagwe Mutahi Kagwe

Kenya siku ya Jumapili ilisajili visa 685 vipya vya maambukizi ya Covid-19 kutokana na sampuli 4,912 zilizopimwa chini ya saa 24  kufikisha idadi ya jumla ya visa 44,881 vya maambukizi.

Kati ya maambukizi haya mapya 635 ni wakenya huku 50 wakiwa raia wa kigeni, 456 ni wanaume huku 229 wakiwa wanawake.

 

Waziri wa afya Mutahi Kagwe alisema mhasiriwa wa umri wa chini zaidi ana umri wa mwaka mmoja huku mwenye umri wa juu akiwa na miaka 99.

Mutahi aliwahimiza viongozi hasa wanasiasa kufuata kanuni za wizara ya afya na kuwa mfano mwema kwa wananchi.

"Hii leo watu 28 wamo katika hali mahututi kufuatia maambukizi ya corona," Kagwe alisema.

Vile vile watu 105 walipoma hivyo siku ya Jumapili na kufikisha jumla ya watu 31,857 waliopona. 73 walikuwa wakipokea matibabu wakiwa nyumbani na 32 katika hospitalini.

Watu saba wameaga dunia kutokana na corona na kufikisha idadi ya jumla ya watu 832.

(Mhariri Davis Ojiambo)