• Upande wa mashtaka uliomba mahakama kuwaruhusu mashahidi wawili kutoka idara ya Ulinzi kutoa ushahidi wao kwa faragha.
Mahakama mjini Nairobi imeruhusu kusikizwa faraghani kwa kesi dhidi ya aliyekuwa waziri wa michezo Rashid Echesa.
Hii ni baada ya upande wa mashtaka kuiomba mahakama kuwaruhusu mashahidi wawili kutoka Wizara ya Ulinzi kutoa ushahidi wao kwa faragha.
"Kwa kuwa hakuna pingamizi mashahidi ambao wataitwa watatoa ushahidi faraghani," mahakama iliamua.
Katika kesi inayohusu zabuni bandia ya silaha za kijeshi, Echesa na wengine wanne wameshtakiwa kwa makosa ya jinai.
Echesa alikana mashtaka yote zaidi ya 10 yanayohusiana na ulaghai katika zabuni bandia ya silaha.
Echesa ambaye ni mwandani wa naibu rais William Ruto alipigwa kalamu na rais Uhuru Kenyatta mwaka 2019 kutoka baraza la mawaziri kwa sababu ambazo hazikutajwa.