Wetangula ashinda Useneta Bungoma kwa mara ya 3 mtawalia

Sasa ni wazi kwamba Bungoma ni ngome ya FORD-K kwa sababu imenyakua nyadhifa tatu za ugavana, mwakilishi wa wanawake na wabunge 3.

Muhtasari

• "Wengi wameuliza kwa nini ninatetea kiti changu licha ya kupata 30% katika serikali ya Kenya Kwanza," - Wetangula.

• Sitafuti faida za kibinafsi, faida ambazo tumepata katika mkataba wa Kenya Kwanza zitagawanywa katika serikali," Wetangula alisema.

Moses Wetangula
Moses Wetangula

Seneta wa sasa wa Bungoma Moses Wetangula amefanikiwa kutetea kiti chake cha useneta Bungoma kwa mara ya tatu mtawalia ambapo alikuwa akigombea kwa tiketi ya chama chake cha FORD-Kenya.

Kinara huyo wa Muungano wa Kenya Kwanza amewathibitishia wakosoaji wake kuwa ni kweli kaunti ya Bungoma ni ngome yake licha ya awali eneo hilo kusemekana kwamba ni ngombe ya mshindani wao mkuu Raila Odinga wa Azimio la Umoja One Kenya.

Kuhusu ni kwa nini alikuwa akiwania nafasi ya useneta baada ya kuahidiwa kuajiriwa kama spika ikiwa Kenya Kwanza itatwaa serikali, alisema hakuwania kwa sababu za kibinafsi bali kwa takwa la wenyeji wa Bungoma.

"Wengi wameuliza kwa nini ninatetea kiti changu licha ya kupata 30% katika serikali ya Kenya Kwanza, sitafuti faida za kibinafsi, faida ambazo tumepata katika mkataba wa Kenya Kwanza zitagawanywa katika serikali," Wetangula alisema.

Wanachama wa chama hicho chenye nembo ya simba walijaribu kumwondoa Wetangula kutoka nafasi yake ya uongozi na kabisa kutoka kwa chama cha FORD-K.

Gavana Wangamati, Wafula Wamunyinyi wa DAP-K na Eseli Simuyu walikuwa wachochezi wakuu wa kuondolewa kwake madarakani. Wote Waliopanga njama ya kumtimua madarakani sasa wameshindwa katika uchaguzi uliokamilika Agosti 9.

"Nilikuambia kwamba wale waliopanga mapinduzi hawataning’atua kutoka FORD-Kenya, niliwaahidi kwamba lazima washindwe katika chaguzi hizi ambazo zimetokea, mapinduzi yao yalikufa walipofika," Wetang'ula alisema.

Sasa ni wazi kwamba Bungoma ni ngome ya FORD-K kwa sababu imenyakua nyadhifa tatu za ugavana, mwakilishi wa wanawake na wabunge 3. John Makali wa FORD-Kenya alimuangamiza Wafula Wamunyi wa DAP-K katika eneo bunge la Kanduyi, Martin Wanyonyi wa chama cha FORD-K alimshinda Wanjala Iyaya wa DAP-K kunyakua kiti cha mbunge wa Webuye Mashariki, ambapo aliweka rekodi ya kuwa mlemavu wa Ngozi wa kwanza kabisa kuwahi kuchaguliwa kupitia kura ya debeni tangu uhuru wa Kenya ulipopatikana miaka ya sitini.

Pia katika eneo bunge la Kabuchai, Majibo Kalasinga wa FORD-Kenya alimshinda Evans Kakai wa Jubilee, na kuweka muhuri wa kudumu wa Wetangula na chama chake kuzidi kunguruma katika kaunti hiyo ya mkoa pana wa Magharibi.