"Kama Nilikosea Mtu Yeyote Naomba Mnisamehe" - Profesa George Magoha

"Hakuna mtu ambaye ni mkamilifu,” - profesa Magoha

Muhtasari

• "Ikiwa ucheshi wowote kati ya hivyo ulikwenda kinyume, hiyo haikuwa nia na naomba radhi kwa umma" - Magoha.

Waziri wac elimu profesa George Magoha
Waziri wac elimu profesa George Magoha
Image: THE STAR//MAKTABA

Huku muda ukiwa umeyoyoma kwa serikali ya Jubilee na baraza lake la mawaziri kufungasha virango vyao na kuondoka nyumbani, mipango mbali mbali imeanza kuwekwa tayari ili kuwarahisishia mawaziri wapya watakaoteluliwa na serikali ijayo inayotarajiwa kuongozwa na rais mteule William Ruto iwapo muungano wa Azimio la Umoja One Kenya ukiongozwa na Raila Odinga hautawasilisha kesi mahakamani kupinga ushindi wake.

Mmoja kati ya mawaziri ambao kwa mara kadhaa wamekuwa wakidokeza kwamba hawatoendelea katika nyadhifa zao za uwaziri ni profesa George Magoha anayesimamia wizara ya elimu.

Waziri Magoha katika kipindi ambacho amehudumu kama Waziri kwa takriban miaka minne, amekuwa ni chukizo la wengi na vile vile kipenzi cha wengi kwa viwango sawa.

Jumatano alipokuwa akizungumza katika shule ya msingi ya Mwangaza, Kayole jijini Nairobi akizindua mkumbo wa pili wa ujenzi wa madarasa ya mtaala mpya wa CBC alitoa wito kwa wote ambao huenda aliwakosea kwa kuburuzana mabega nao wakati akiwa kazini kumsamehe kwani hakuna aliye mkamilifu chini ya jua.

“Imekuwa si rahisi kuwa waziri wa elimu na ili kusonga mbele, nimekuwa imara sana na wakati mwingine imara sana kati ya uimara ambao mtu anaweza kusema nilianza utani. Nataka kusema kwamba ikiwa ucheshi wowote kati ya hivyo ulikwenda kinyume, hiyo haikuwa nia na naomba radhi kwa umma. Hakuna mtu ambaye ni mkamilifu,” profesa Magoha alisema.

Waziri huyo ambaye amejipata katika mzozo mkali haswa na makundi yanayotetea haki za mashoga na pia kundi lile lisiloamini katika uwepo wa Mungu alisema kwamba ilimbidi kuchukua misimamo mikali dhidi ya mambo mengine ambayo Imani yake ilimuusia kuwa si sahihi na pia kuwataka wote ambao walikwasika na maamuzi yake kumsamehe ila akasisitiza kwamba misimamo hiyo itasalia na hawatolegeza Kamba hivi karibuni.

“Ninaheshimu kila mtu kutoka chini hadi juu. Ninapata ujasiri wangu kwanza kutoka kwa Mungu na pili kutoka Starehe Boys Training Centre. Sisi ni tai na tunaruka juu, na hatuogopi, na tunafanya kazi kama tai hata kama hautupendi. Ikiwa wakati wa mchakato huo tulionekana kana kwamba tuna kiburi, basi tunaomba msamaha wako, lakini sio kwamba tunakaribia kubadilika. Tai wanaendelea kuruka na tai wakiruka hupotea tu angani, ndicho kitakachotokea kwetu,” Waziri Magoha alisema.