Patanisho: Jamaa aachwa kwa sababu babake ni mganga, mkewe amwagiza atafute mwingine

"Nilimpeleka nyumbani. Hakutaka kukaa na babangu kwa sababu ni mganga," Oscar alisema.

Muhtasari

•Oscar alisema mkewe aligura ndoa yao ya miaka miwili kwa sababu hakupenda kuishi pamoja na baba yake ambaye ni mganga.

•Oscar alisistiza kuwa hakuna kosa lingine ambalo alimtendea mkewe  likachangia kutoroka kwake.

Ghost na Gidi
Ghost na Gidi
Image: RADIO JAMBO

Katika kipindi cha Gidi na Ghost asubuhi kitengo cha Patanisho, jamaa aliyejitambulisha kama Oscar alituma ujumbe akiomba kupatanishwa na mke wake Martha ambaye alimwacha kwa sababu hakupenda taaluma ya baba yake.

Oscar alisema mkewe aligura ndoa yao ya miaka miwili kwa sababu hakupenda kuishi pamoja na baba yake ambaye ni mganga.

"Tumekaa na mke wangu miaka miwili. Nilimpeleka nyumbani. Hakutaka kukaa na babangu kwa sababu ni mganga," alisema.

Aliongeza, "Tukawa tunakorofishana akarudi kwao. Juzi aliandikia ujumbe akaniambia nitafute mke mwingine.Nilimwambia anitafutie kwani siwezi kupata mwanamke ."

Oscar alidai kuwa baba yake alitaka aridhi kazi yake ya uganga, jambo ambalo yeye na mkewe hawakupendelea.

"Baba alisema mke wangu ndiye alikuwa anafanya nikatae kazi yake. Alitaka niridhi kazi  yake  naye mke wangu alikuwa ananiambia niingie kwenye mambo ya kanisa. Baba hawako pamoja na mama," alisema.

Oscar alisistiza kuwa hakuna kosa lingine ambalo alimtendea mkewe  likachangia kutoroka kwake.

"Baada ya kunitumia ujumbe hachukui simu zangu. Bado ako kwao" alisema.

Juhudi za kuwapatanisha Oscar na mkewe ziliangulia patupu kwani Martha alikata simu mara moja punde baada ya Gidi kumweleza sababu ya kumpigia. Oscar alisema kuwa haelewi kabisa kinachofanya mkewe asitake kunena naye.

Oscar alipopatiwa nafasi ya kuzungumza na Martha hewani alimhakikishia upendo wake mkubwa kwa na kumuomba arejee nyumbani

"Nilikuwa nimepata kazi tungekaa pamoja tuanzishe maisha. Si vizuri umeniweka parking,"