Milio ya risasi yavuruga upigaji kura Ugenya, msaidizi wa chifu akijeruhiwa

Wanaume wanne walimvamia msimamizi, na kumtaka aondoke katika kituo cha kupigia kura kwani uwepo wake ungewashawishi wapiga kura.

Muhtasari

• Ogola alisema alikuwa ametoka kupiga kura muda mfupi baada ya saa kumi na mbili asubuhi wakati watu wanne, miongoni mwao kakake mwanasiasa, walipomkabili.


• Juhudi za polisi kuleta utulivu hazikufua dafu na kuwalazimu kupiga risasi hewani.

Pingu
Image: Radio Jambo

Wapiga kura waliojizatiti asubuhi katika kituo cha Bar Ndege huko Ugenya walitoroka kwa usalama baada ya milio ya risasi kutanda muda mfupi baada ya kituo kufunguliwa kwa ajili ya kupiga kura.

 

Kulingana na mashahidi walioshuhudia, maafisa wa usalama waliokuwa wakisimamia kituo hicho walilazimika kufyatua risasi hewani ili kumwokoa chifu msaidizi wa eneo hilo dhidi ya maajenti wa mgombea ubunge aliyemtaka msimamizi kuondoka ukumbini.

 

Msaidizi wa chifu wa lokesheni ndogo ya Kathieno “B” katika wadi ya Ugenya Mashariki, Joash Ogola, alikuwa wa kwanza kwenye foleni na alikuwa ametoka kupiga kura kisa hicho kilipotokea.

 

Ogola alisema alikuwa ametoka kupiga kura muda mfupi baada ya saa kumi na mbili asubuhi wakati watu wanne, miongoni mwao ndugu wa mwanasiasa huyo, walipokabiliana na kuanza kumshinikiza aondoke ukumbini mara moja.

 

Chifu huyo msaidizi alisema kuwa vijana hao walidai kuwa kuwepo kwake katika eneo hilo kungeathiri wapiga kura kumuunga mkono mpinzani wao.

 

Makabiliano hayo yalizua mkanganyiko katika kituo cha kupigia kura, na kuwavutia vijana kadhaa ambao walishuka kwa chifu.

 

Juhudi za polisi kuleta utulivu hazikufua dafu na kuwalazimu kupiga risasi hewani.

 

Chifu Ogola, ambaye aliokolewaa Kwenda eneo salama, alisema alipata majeraha kwenye mguu wake wa kulia.

 

Kamanda wa polisi wa kaunti ndogo ya Ugenya Benard Wamugunda alithibitisha kisa hicho akisema polisi wameanzisha uchunguzi.

 

Wamugunda aliwahakikishia wakazi usalama wa juu zaidi, na kuongeza kuwa hatua zitachukuliwa dhidi ya yeyote aliyehusika katika tukio hilo.

 

Tukio hilo limekuja kufuatia tukio lingine, ambapo gari lililokuwa na mapanga na marungu lilizuiliwa na polisi katika kituo cha biashara cha Siranga jimbo la Ugenya mara baada ya wafuasi wa wagombea wawili wa ubunge waliokuwa wakichuana katika mapambano yaliyosababisha watu kadhaa kujeruhiwa.

 

Wakati huo huo, upigaji kura ulianza vizuri katika kaunti ya Siaya, huku vituo vikifunguliwa saa kumi na mbili asubuhi.

 

Ingawa zoezi hilo lilikuwa likiendelea, wapiga kura wachache walilalamikia kasi ndogo ya kuwatambua wapiga kura na kutaka matumizi ya rejista ya mwongozo kuharakisha mchakato huo.

 

Foleni ndefu zilirekodiwa katika vituo vingi vya kupigia kura saa za asubuhi. Majengo ya biashara katika mji wa Siaya yalifungwa huku wakaazi wakimiminika katika kituo cha kupigia kura kuwachagua viongozi wao.

 

Barabara katika mji huo zilibaki bila watu, isipokuwa watu wachache waliokuwa wakihamia au kutoka vituo vya kupigia kura.

Tafsiri na MOSES SAGWE